
Picha hii ya faili isiyo na tarehe inaonesha mandhari ya Kituo cha Umeme wa Upepo cha Aysha II katika Jimbo la Somali, Ethiopia. (Dongfang Electric Corporation/Handout kupitia Xinhua)
Waziri Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed, siku ya Jumamosi alizindua awamu ya kwanza ya Kituo cha Umeme wa Upepo cha Aysha II katika Jimbo la Somali, akisisitiza kuwa maendeleo ya nishati safi ni nguzo muhimu ya mabadiliko ya muda mrefu ya kiuchumi ya nchi hiyo.
Akizungumza katika hafla hiyo, iliyohudhuriwa na Rais Ismail Omar Guelleh wa Djibouti na Rais Hassan Sheikh Mohamud wa Somalia, Abiy alisema Kituo cha Umeme wa Upepo cha Aysha II kinaakisi dhamira ya Ethiopia ya kujitegemea kupitia matumizi madhubuti ya rasilimali za ndani.
Picha hii ya faili isiyo na tarehe inaonesha mandhari ya Kituo cha Umeme wa Upepo cha Aysha II katika Jimbo la Somali, Ethiopia. (Dongfang Electric Corporation/Handout kupitia Xinhua)
“Ningependa kutoa shukrani zangu kwa Shirika la Umeme la Ethiopia (EEP), Dongfang Electric Corporation, kampuni ya Kichina iliyotekeleza mradi huu, pamoja na wananchi wa eneo hili kwa mchango wao katika kukamilika kwa mafanikio kwa awamu ya kwanza ya mradi,” alisema Abiy.
Akibainisha kuwa maendeleo ya nishati safi nchini Ethiopia yataimarisha ushirikiano wa kikanda na muunganiko wa kuvuka mipaka, Abiy alisema kuwa mafanikio ya Ethiopia katika ukuaji na maendeleo ya nishati hayawezi kuhakikishwa bila ushirikiano na nchi jirani.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa EEP Ashebir Balcha, mradi wa Aysha II ulioanzishwa mwaka 2017 utakuwa na uwezo wa jumla wa megawati 120, huku megawati 80 kutoka awamu ya kwanza tayari zikiwa zimeunganishwa kwenye gridi ya taifa.
Picha hii ya faili isiyo na tarehe inaonesha mandhari ya Kituo cha Umeme wa Upepo cha Aysha II katika Jimbo la Somali, Ethiopia. (Dongfang Electric Corporation/Handout kupitia Xinhua)
“Jimbo la Somali lina rasilimali nyingi za upepo, nishati ya jua na gesi asilia. Serikali itazindua hivi karibuni miradi miwili ya mashamba ya upepo katika maeneo ya karibu, yenye uwezo wa kuzalisha megawati 300 na 350 za umeme mtawalia,” alisema Balcha.
Baada ya kukamilika, Kituo cha Umeme wa Upepo cha Aysha II kitakuwa na jumla ya mitambo 48 ya upepo, ambapo 32 tayari zinafanya kazi, kila moja ikizalisha umeme wa megawati 2.5.
Moges Mekonnen, mkurugenzi wa mawasiliano wa EEP, aliiambia Xinhua kuwa Dongfang Electric Corporation imeanzisha teknolojia na miundo mipya ambayo haijawahi kutumika katika miradi mitatu ya awali ya mashamba ya upepo nchini Ethiopia.
“Kila kinu cha upepo katika mradi wa Aysha II kina uwezo wa juu wa kuzalisha megawati 2.5, kiwango ambacho ni angalau megawati moja zaidi ya uwezo wa kila kinu cha upepo katika mashamba mengine ya upepo nchini,” alisema Mekonnen.




