Fahamu utajiri wa waliopendekezwa kuwa mawaziri ambao walipigwa msasa Agosti 1

Uhakiki wa wateule wa Baraza la Mawaziri ulianza Bungeni Alhamisi, Agosti 1, 2024.

Muhtasari

•Wakiwa mbele ya kamati hiyo, wateule wa baraza la mawaziri wote walihitajika kutangaza thamani yao ya sasa.

•Uhakiki wa walioteuliwa utaendelea kwa siku nne kuanzia Agosti 1, 2024 hadi Jumapili, Agosti 4, 2024.

walipigwa msasa Agosti 1, 2024.
Kindiki Kithure, Alice Wahome, Deborah Mulongo, Soipan Tuya na Julius Ogamba walipigwa msasa Agosti 1, 2024.

Uhakiki wa wateule wa Baraza la Mawaziri ulianza Bungeni Alhamisi, Agosti 1, 2024.

Mteule wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Kithure Kindiki alikuwa wa kwanza kupigwa msasa na kamati kuhusu uteuzi.

Mteule huyo alifika katika Majengo ya Bunge dakika chache kabla ya saa mbili asubuhi. Uhakiki ulipangwa kuanza saa mbili asubuhi, hata hivyo, ulicheleweshwa na ulianza saa mbili unusu asubuhi.

Mteule wa Wizara ya Afya, Deborah Mulongo Barasa alikuwa wa pili kupigwa msasa na Kamati ya Uteuzi ya Bunge la Kitaifa.

Alice Wahome wa wizara ya ardhi alifuatwa mwendo wa saa sita adhuhuri , Migos Ogamba wa elimu akaingia saa tisa alasiri, na Soipan Tuya wa Ulinzi alifunga siku hiyo mwendo wa saa kumi na moja jioni.

Wakiwa mbele ya kamati hiyo, wateule wa baraza la mawaziri, waliohudumu katika baraza la mawaziri lililovunjwa na wale ambao wameteuliwa hivi majuzi, wote walihitajika kutangaza thamani yao ya sasa.

Hii hapa orodha ya thamani halisi iliyotangazwa na wateule mbalimbali;

  • Kithure Kindiki (Usalama wa Ndani), Sh544m, kutoka Sh694m mnamo Oktoba 2022.
  • Alice Wahome (Ardhi, kazi za umma), Sh327m kutoka Sh218m mnamo Oktoba 2022.
  • Soipan Tuya (Ulinzi), Sh243.4m, kutoka Sh156m mnamo Oktoba 2022.
  • Deborah Barasa (Afya), Sh455.8m
  • Julius Ogamba (Elimu), Sh790m

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa mwezi uliopita, uhakiki wa walioteuliwa utaendelea kwa siku nne, ambapo angalau wateule watano watapigwa msasa kuanzia Alhamisi, Agosti 1, 2024 hadi Jumapili, Agosti 4, 2024.

Mnamo Agosti 2, kamati itawapiga msasa  Andrew Mwihia (Kilimo) saa mbili asubuhi, Aden Duale (Mazingira) saa nne asubuhi, Eric Muuga (Maji), Davis Chirchir (Uchukuzi) na Margaret Ndung’u (ICT).

Mnamo Agosti 3, John Mbadi (Hazina), Salim Mvurya (Biashara), Rebecca Miano (Utalii) saa sita adhuhuri, Opiyo Wandayi (Nishati) saa tisa alasiri na Kipchumba Murkomen (Michezo) watatokea mbele ya  kamati ya uhakiki.

Mnamo Agosti 4, Hassan Joho (Madini), Alfred Mutua (Kazi), Wycliffe Oparanya (Ushirika), Justin Muturi (Utumishi wa Umma) na Stella Lang'at (Jinsia) watapigwa msasa..