Sakaja abubujikwa na machozi akizindua wa mpango wa kuwapa wanafunzi chakula

"I'm sorry your excellency but ni uchungu ya hawa watoto wanakosa chakula," sakaja alisema.

Muhtasari

• Sakaja alisimama kwa muda huku akitokwa na  machozi, akisimulia jinsi mpango huo ulivyokuwa muhimu kwake.

•  Mpango huo wa kila mwaka wa shilingi bilioni 1.2 ni sehemu ya mpango wa Sakaja wa Kulisha Shule—Dishi na County.

Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja akipanguzwa machozi na MCA wa Mlango Kubwa Susan Makungu huku akimwaga machozi Roysambu, Nairobi mnamo Juni 20, 2023.
Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja akipanguzwa machozi na MCA wa Mlango Kubwa Susan Makungu huku akimwaga machozi Roysambu, Nairobi mnamo Juni 20, 2023.
Image: SCREENGRAB

Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja alitokwa na machozi huku akizindua mpango wa chakula kwa wanafunzi katika kaunti ya Nairobi.

Akizungumza katika mtaa wa Roysambu siku ya Jumanne,bosi huyo wa kaunti alidodokwa na machozi alipokuwa akizungumzia mpango wake wa Dishi na County unaokusudia kuwalisha wanafunzi wa Nairobi.

Akitoa hotuba yake mbele ya Rais William Ruto, Sakaja alisimama kwa muda huku akitokwa na  machozi, akisimulia jinsi mpango huo ulivyokuwa muhimu kwake.

"I'm sorry your excellency but ni uchungu ya hawa watoto wanakosa chakula," sakaja alisema.

Sakaja alimpongeza Rais kwa kuunga mkono mpango wake wa kuwalisha wanafunzi wa kaunti ya Nairobi.

"Vile watu wanakumbuka maziwa ya nyayo watu watakumbuka chakula ya Ruto." 

Itaigharimu shilingi tano kwa wanafunzi wanaosoma katika shule za umma katika kaunti ya Nairobi pamoja na wale wa ECDE kupata chakula kilichopunguzwa bei katika mwaka wa kifedha 2023/2024.

Mpango huo wa kila mwaka wa shilingi bilioni 1.2 ni sehemu ya mpango wa Sakaja wa Kulisha Shule—Dishi na County.

Siku ya Jumatatu, msingi wa ujenzi wa jikoni kuu ulifanyika katika gatuzi ndogo  10 za kaunti ya Nairobi.

Ujenzi huo unatarajiwa kuchukua takriban wiki 10 huku mlo wa kwanza ukitolewa katika siku ya kwanza ya muhula wa tatu wa mwaka huu.

Baaadhi ya gatuzi ndogo zitakazojengwa jikoni hizi ni pamoja na Dagoretti Kaskazini, Embakasi ya Kati, Embakasi Kusini, Kasarani, Kibra, Makadara, Starehe, Roysamu, Ruaraka, na kaunti ndogo za Westlands.

Gavana Sakaja alisema mradi huo ni sehemu ya maono aliyokuwa nayo kwa miaka mingi, kuhakikisha upatikanaji wa chakula cha kila siku chenye lishe bora kwa watoto wote katika shule za msingi za umma na vituo vya umma vya Masomo ya Awali(ECDE).