Julius Malema aunga mkono maandamano ya Gen Z wa Kenya

Chama cha Malema kimeongeza kuwa taasisi hizo za kimataifa ndizo sababu ya kuenea kwa umaskini na machafuko ya kijamii barani Afrika.

Muhtasari

•Chama cha EFF kinachoongozwa na Julius Malema kimetoa taarifa ya kuunga mkono maandamano dhidi ya mswada wa fedha.

•Chama hicho kimetaka serikali ya Kenya kutotumia nguvu kuwadhibiti waandamanaji ambao wanatafuta haki yao.

Kiongozi wa chama cha EFF nchini Afrika Kusini
Julius Malema Kiongozi wa chama cha EFF nchini Afrika Kusini
Image: BBC

Chama cha Economic Freedom Fighters (EFF) cha Afrika Kusini kinachoongozwa na kiongozi wa upinzani Julius Malema, kimewapongeza Wakenya kwa kuandamana kupinga Mswada mbaya wa Fedha wa 2024.

Katika taarifa siku ya Jumatatu, EFF ilibainisha kuwa wanasimama kwa mshikamano na vijana wa Kenya ambao wameingia mitaani kupinga mswada wa fedha.

Huku likishutumu shirika la fedha la kimataifa (IMF) na benki ya dunia kwa kuunga mkono katika mapendekezo hayo, chama hicho kilikiri kuwa mswada huo utazidi kuzorotesha gharama za maisha na uchumi wa taifa.

"Mswada wa sheria ya fedha wa 2024 ni matokeo ya pendekezo kutoka kwa Shirika la fedha la kimataifa (IMF) na benki ya dunia kwa serikali ya Kenya. Kwa hivyo, hii ni sehemu ya tatizo kubwa linalokabili mataifa mengi yanayoendelea chini ya nira ya IMF na Dunia. Mikopo ya benki.."  taarifa hiyo  ilisomeka.

Chama cha Malema kimeongeza kuwa taasisi hizo za kimataifa ndizo sababu ya kuenea kwa umaskini na machafuko ya kijamii barani Afrika ili kuhalalisha kuanzishwa kwa vituo vya kijeshi vya Marekani katika bara hilo.

EFF ilibainisha kuwa wanaunga mkono kikamilifu maandamano nchini Kenya wakiwataka waandamanaji kutolegea katika kupigania haki ya kiuchumi. Pia waliitaka serikali ya Kenya kuacha kutumia nguvu wakati wa maandamano ya amani.

"Matumizi ya mabomu ya machozi, maji ya kuwasha na risasi za mpira dhidi ya raia wanaotumia haki yao ya kuandamana hayakubaliki," chama hicho kilisema.

"Tunaitaka serikali ya Kenya kuwasimamisha polisi na kuheshimu haki ya watu ya kukusanyika kwa amani. Wale wote ambao wamekamatwa wanapaswa kuachiliwa mara moja."

Maandamano hayo yalianza Juni 17 na yanatazamiwa kushika kasi wiki hii ili kuongeza shinikizo kwa wabunge wa Kenya kuutupilia mbali Mswada huo.