logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Ikiwa Mungu ataniambia nifunge macho niombe kitu kimoja, nitaomba kuwa Gen Z – Moses Kuria

Kuria pia alizungumzia suala la kukejeliwa mitandaoni baada ya baraza la mawaziri kuvunjwa na rais mnamo Julai 11.

image
na Radio Jambo

Habari15 July 2024 - 07:17
MOSES KURIA

Aliyekuwa waziri wa utumishi wa umma, utendakazi, Moses Kuria ameanza kujuta kwa kile alisema ni kuwadharau vijana wa Gen Z ambao maandamano yao yalimpelekea kupoteza kazi kama waziri wiki jana.

Akizungumza na runinga ya Citizen, Kuria alisema kwamba alikuwa anawapuuza vijana wa Gen Z katika mtandao wa X lakini mwisho wa siku shinikizo zao zilimpelekea rais kulivunja baraza lake la mawaziri.

Kuria anasema kwamba katika maisha yake ya baadae kama atapata nafasi Mungu kumuuliza angependa kuwa nini, basi bila kusita atachagua kuwa Gen Z.

“Nimekuwa nikiwaita kizazi cha Uber na vidole vya samaki, wamenithibitishia kuwa sikuwa sahihi. Sasa wale watu nilikuwa naitwa kizazi cha uber na vidole vya samaki wamenionyesha kwamba wanaweza kuwa injini ya maana ya kulipeleka taifa mbele na kulirudisha kwenye njia salama. Kusema ukweli kama Mungu angeniambia nifunge macho yangu na nifanye ombi moja, ningeomba kuwa Gen Z,” Kuria alisema.

Moses Kuria alisema kwamba anaunga mkono mia kwa mia hatua ya rais kulivunja baraza la mawaziri, akisema kwamba kulikuwa na nyufa nyingi ambazo zilikuwa hata zinafanya kuwa vigumu kwa mikutano ya baraza la mawaziri kufanyika.

“Ni kweli tulikuwa na matatizo, hata kwa kufanya mikutano ya baraza la mawaziri ilikuwa ni shida, na ningependa kumpa rais nafasi ya kuunda upya  baraza lake la mawaziri, na kwa wenzangu, ningesema kwamba hatufai hata kusoneneka kwa lolote. Nafikiri nilimhurumia sana rais, na alikuwa ni lazima afanye chenye kilistahili kufanyika. Kama ni mimi kuachia nafasi yenye nilikuwa nashikilia ili tuwe na taifa, basi na iwe hivyo,” alisema.

Kuria pia alizungumzia suala la kukejeliwa mitandaoni baada ya baraza la mawaziri kuvunjwa na rais mnamo Julai 11.

“Naona watu wanani’enjoy eti ooh wewe ulifutwa, na hata hao wanajua, mimi ningependa kujizungumzia na kuzungumzia wengine, mimi sina majuto hata kidogo. Mimi huwezi nikuta kwenye kona eti ninalia kwa kupoteza kazi, hapana, mimi ni mtu wa kimataifa,” alisema.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved