logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mshauri wa Raila, Jakakimba ajiuzulu ODM siku chache baada ya Winnie Odinga kumtusi

Jakakimba hata hivyo alimsifia Odinga akifichua kwamba walikutana mwaka 2004.

image
na Radio Jambo

Makala18 March 2023 - 09:57

Muhtasari


• Licha ya kuonekana kutofautiana vikali na binti wa Odinga, Jakakimba alimsifia pakubwa Odinga kwa kumkuza na kumlea kisiasa tangu 2004.

• Jakakimba amekuwa mshauri wa karibu wa kisiasa wa Raila Odinga na kwa wakati mmoja aliwahi kuwa kama msaidizi wake wa kibinafsi.

Silas Jakakimba

Mwanasiasa Silas Jakakimba, mshirika wa Raila Odinga, amejiuzulu kama mwanachama wa maisha wa chama cha ODM, siku mbili tu kuelekea maandamano ya Jumatatu dhidi ya serikali ya William Ruto.

Jakakimba ambaye kwa muda mrefu amekuwa akihudumu kama msaidizi wa karibu wa Odinga aliandikia msajili wav vyama vya kisiasa barua ya kutaka kuondolewa kutoka sajili ya wanachama wa ODM, mara moja.

"Naomba utimize uamuzi huu kwa kufuta jina langu kwenye daftari rasmi la wanachama wa ODM," sehemu ya barua yake kwa ORPP ilisema.

Katika barua hiyo yenye maelezo marefu na ambayo yalikuwa yanamsifia na kumvisha koja la maujai ghali bwana Odinga, Jakakimba alifichua kwamba mara ya kwanza walikutana na Odinga mwaka 2004 na mpaka sasa amemlea na kumkuza pakubwa katika fani nyingi za maisha.

"Kwa shukrani na heshima nyingi, Jakom, pokea uhakikisho wa heshima yangu ya juu, kuzingatia na maombi kwa ajili ya afya yako nzuri na maisha marefu ya furaha. Nimebahatika kushiriki katika fahari adimu ambayo nimekuwa pamoja nanyi huku mkipeana changamoto kadhaa kuona marekebisho ya usanifu wa utawala wetu wa wakati huo na kuwa utawala wa katiba mpya ulioratibu ugatuzi katika kitovu cha utawala wetu," alisema.

Hadi kujiuzulu kwake, mwanasiasa huyo alikuwa akihudumu kama mshauri wa Bw Odinga. Mnamo 2007, alihudumu kiongozi wa ODM kama msaidizi wake wa kibinafsi bungeni.

Kujiuzulu kwake kunakuja siku chache tu baada ya kupapurana mitandaoni na binti wa Raila Odinga, Winnie Odinga.

Jakakimba alilalamika vikali kwenye ukurasa wake wa Twitter jinsi Winnie alimtumia neno la matusi kwa kile alisema kwamba ni kutokana na uamuzi wake wa kutumia picha ya pamoja akisalimiana na rais Ruto kwenye jalada lake Twitter.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved