Ruhusu wabunge wa upinzani kufanya kazi na Ruto - Murkomen amwambia Raila

Haya yanajiri baada ya Raila kuidhinisha kutimuliwa kwa wabunge watano wa ODM ambao walikuwa wamebadili utiifu kwa Rais hadharani.

Muhtasari
  • Raila aliwataja waasi hao kuwa wasaliti akiongeza kuwa kuna njia mwafaka za kushirikiana na serikali ya Kenya Kwanza
  • Murkomen alisema Raila anafaa kuwaacha wanachama wanaotaka kufanya kazi na serikali wafanye hivyo badala ya kuwaadhibu.

Waziri wa Barabara na Uchukuzi Kipchumba Murkomen amemtaka kiongozi wa upinzani Raila Odinga kuwaruhusu wabunge wa chama cha ODM kufanya kazi na serikali.

Murkomen alisema Raila anafaa kuwaacha wanachama wanaotaka kufanya kazi na serikali wafanye hivyo badala ya kuwaadhibu.

Haya yanajiri baada ya Raila kuidhinisha kutimuliwa kwa wabunge watano wa ODM ambao walikuwa wamebadili utiifu kwa Rais hadharani.

Hata hivyo, Murkomen alisema ikiwa Raila ameafikiana kuhusu mazungumzo kati ya serikali na upinzani, anafaa pia kuruhusu ushirikiano kwa maendeleo ya nchi.

"Ulisema tunapaswa kuketi na kuzungumza lakini sasa kuna wengine ambao wanaadhibiwa katika chama kwa sababu ya kukaa chini na rais," Murkomen alisema.

"Ikiwa tumekubaliana kwamba tutaketi pamoja kwa madhumuni ya maendeleo na kila mtu ana haki ya kukutana na rais na CS Murkomen, kwa hivyo, sitaki mtu yeyote apelekwe kortini ya ODM kwa kukaidi maagizo ya kuketi nasi.

“Nataka kufanya kazi nanyi watu kwa muda mrefu katika dunia hii, hasa katika masuala yanayohusu Wizara yangu. Kwa hivyo Raila, acha watu hawa tunafanya kazi pamoja kwa sababu ni sehemu ya nia njema.

Wabunge waliofurushwa kutoka kwa chama hicho ni pamoja na Elisha Odhiambo (Gem), Caroli Omondi (Suba Kusini), Gideon Ochanda (Bondo), Phelix Odiwuor (Lang’ata) na Seneta wa Kisumu Prof Tom Ojienda.

NEC ilikiagiza chama kuwatimua watano hao kwenye daftari lao baada ya kuendeleza maslahi ya vyama pinzani vya kisiasa.

Raila aliwataja waasi hao kuwa wasaliti akiongeza kuwa kuna njia mwafaka za kushirikiana na serikali ya Kenya Kwanza