Jamaa apoteza kazi ya Sh303K baada ya rafiki aliyesaidia kupata kazi kumripoti kwa bosi

Rafiki huyo walijuana baada ya kuingia kwenye DM yake na kumuomba kumnusuru kutoka kwa lindi la mawazo kutokana na kukosa kazi kwa muda mrefu.

Muhtasari

• Ufichuzi huo ulisababisha kufutwa kazi kwa rafiki yake lakini msaliti huyo pia hakupewa kazi hiyo.

• Hadithi yake ilishirikiwa na rafiki mwingine wa kike kwenye TikTok na  ilizua tafrani kwenye jukwaa.

Mwanamume mwenye huzuni na mfadhaiko.
Mwanamume mwenye huzuni na mfadhaiko.
Image: Maktaba

Mwanamume mmoja amepeleka katika mitandao ya kijamii kulalamika akidai kwamba rafiki aliyemsaidia kumuunganisha na ajira alimgeuka na kuenda kumripoti kwa bosi yake.

Mwanamume huyo alisema kwamba kilichomuuma ni kupoteza ajira yake ambayo alikuwa anaingiza mfukoni mshahara wa dola elfu 2 [shilingi laki 3 na elfu 3] kila mwezi.

Tukio hilo lilisimuliwa na rafiki wa mwathirika aliyepoteza kazi katika mtandao wa TikTok.

Alisema kwamba tukio zima lilianzia Twitter, mtumizi wa Twitter, alimfuata rafiki yake kwenye DM yake na kumuelezea jinsi alikuwa anapitia kuzimu na kumuomba kumuunganisha na ajira yoyote mradi kujisitiri kimaisha.

Alimuunganisha na rafiki yake mwingine ambaye alikuwa na kazi ya pembeni ya kuandikia watu wa ughaibuni kazi za mitihani, jambo ambalo alikubali lakini baadae akamgeuka na kumsaliti kwa bosi wake kuhusu kuwa na kazi ya pembeni kando na ile kazi rasmi ya ofisini.

Ufichuzi huo ulisababisha kufutwa kazi kwa rafiki yake lakini msaliti huyo pia hakupewa kazi hiyo. Hadithi yake ilishirikiwa na rafiki mwingine wa kike kwenye TikTok na  ilizua tafrani kwenye jukwaa.