DP Gachagua awasihi Gen Z kusitisha maandamano, “Kile mnasema tunawasikiliza!”

"Hayo mliyoyasema yanatosha hamna haja ya kusema lolote zaidi, Rais, Serikali na kila mtu amewasikia, sasa tusubiri hatua itakayofuata," alisema.

Muhtasari

• "Tafadhali Gen Zs wanangu na binti zangu tafadhali tumewasikia. Mmezungumza waziwazi mlichosema hakihitaji vituo au koma kiko wazi," alisema.

 

DP RIGATHI GACHAGUA
DP RIGATHI GACHAGUA
Image: DPCS

Naibu Rais Rigathi Gachagua amewataka vijana nchini Kenya haswa Gen Zs kukomesha maandamano dhidi ya serikali akiwahakikishia kuwa serikali imesikia na iko tayari kutekeleza matakwa yao.

"Tafadhali Gen Zs wanangu na binti zangu tafadhali tumewasikia. Mmezungumza waziwazi mlichosema hakihitaji vituo au koma kiko wazi," alisema.

Akizungumza katika kaunti ya Kirinyaga siku ya Jumamosi, DP alikiri kuwa ni sawa kwa Wakenya kuandamana na kutafuta majibu kutoka kwa serikali kuhusu masuala ya utawala lakini pia alilalamika kuwa maandamano ya Gen Z yameingiliwa na watu wenye nia ya uhalifu.

Viongozi wengine walioandamana na DP ni pamoja na Njeri Maina, Mwakilishi wa Wanawake wa Kirinyaga, John Kaguchia (Mbunge wa Mukurwe-ini), Seneta Karungo Wa Thang'wa (Kiambu), waliokuwa wabunge Alfred Mwangi Nderitu, Peter Gitau, Kabinga Wachira Thayu na Wangui Ngirichi.

"Lakini mnapotoka kuandamana baadhi ya wahalifu wanajipenyeza kwenye maandamano yenu na kuanza kupora. Hivyo tunataka kuwaomba Gen Zs tafadhali msiruhusu maandamano yenu kutekwa nyara na watu wenye nia ya uhalifu wa kuiba na kuharibu mali," Gachagua alisema.

DP alithibitisha kuwa serikali imesikia malalamishi ya vijana na sasa wanapaswa kuupa utawala wa Kenya Kwanza muda wa kufanyia kazi madai yao.

"Hayo mliyoyasema yanatosha hamna haja ya kusema lolote zaidi, Rais, Serikali na kila mtu amewasikia, sasa tusubiri hatua itakayofuata," alisema.