Jaji Chitembwe akosoa kufutiliwa mbali kwa ushindi wa Uhuru -2017

Muhtasari

• Jaji Chitembwe alidokeza kwamba alikuwa ameshawishika na uamuzi uliopinga wa Jaji Njoki Ndung'u ambapo alikagua fomu zote za na malalamiko yaliyotolewa na kushikilia kuwa uchaguzi ulifanywa kwa mujibu wa sheria.

Jaji Said Chitembwe akipigwa msasa na makamishna wa tume ya JSC
Jaji Said Chitembwe akipigwa msasa na makamishna wa tume ya JSC
Image: JSC

Jaji wa mahakama kuu Said Chitembwe siku ya Jumatatu alikosoa uamuzi wa Mahakama ya Juu uliobatilisha matokeo ya uchaguzi wa urais wa 2017 akisema hakuelewa uamuzi wa wengi.

Uamuzi wa wengi ulifuta uchaguzi wa Rais Uhuru Kenyatta kwa madai kuwa usafirishaji wa matokeo haukufanywa ipasavyo na njia ya uwazi.

Jaji Chitembwe ni mmoja kati ya saba waliotafuta nafasi kuhudumu kama majaji wa Mahakama ya Juu na alikuwa wa kwanza kufika mbele ya jopo la Tume ya Huduma ya Mahakama siku ya Jumatatu kupigwa msasa.

 

Jaji Chitembwe alidokeza kwamba alikuwa ameshawishika na uamuzi uliopinga wa Jaji Njoki Ndung'u ambapo alikagua fomu zote za na malalamiko yaliyotolewa na kushikilia kuwa uchaguzi ulifanywa kwa mujibu wa sheria.

Alihoji pia sababu za Mahakama ya Juu kukataa kushughulikia kesi ya stakabadhi za elimu za Gavana wa Wajir kwa kusema kwamba swala hilo lingeshughulikiwa na tume ya IEBC.

Kulingana na Jaji Chitembwe, korti ilipaswa kuhoji suala hilo kwa sababu imepewa nguvu chini ya sheria kuangalia ikiwa mgombea urais aliteuliwa kwa mujibu wa sheria na ana sifa stahiki.

Alijiuliza ni kwanini korti haikutumia sheria hiyo kushughulikia kesi hiyo katika swala la magavana.

"Ikiwa mgombea aliyesoma tu hadi kidato cha nne ataadhinishwa kugombea ugavana sidhani mikono yangu itafungwa kumuuliza ikiwa ana cheti cha digrii na amepataje," alisema.

Kuhusu suala la ufisadi alisema kwamba ingawa dhana ya umma hayawezi kuondolewa kikamilifu atafanya kazi kuondoa dhana hiyo.

Na kuondoa dhana hiyo kesi za ufisadi zinapaswa kusikilizwa na kuamuliwa kwa muda uliowekwa ili kuhakikisha kuwa hakuna ucheleweshaji wa aina yoyote.

 

Pia alisema majaji wanapaswa kutoa maamuzi yenye busara ili hata wale ambao wamepoteza kesi wasiachwe wakitafakari bali wawe wameelewa sababu za maamuzi.