WIZI SOUTHERN BYPASS

Majambazi 3 wengine wakamatwa kwa kuibia waendesha magari Southern Bypass

Mvulana wa miaka 15 ni miongoni mwa washukiwa watatu waliokamatwa siku ya Jumapili wakipanga njama ya kuvamia wenye magari kutumia silaha aina ya panga

Muhtasari

•Washukiwa 6 walikamatwa wiki iliyopita baada ya kuvamia mwendesha gari mmoja aliyekuwa anasafiri na mwanawe kutoka Nakuru kuelekea Nairobi akitumia bara bara hiyo hiyo.

•Pikipiki mbili walizokuwa wakitumia kutekeleza uhalifu pia zilipatikana na kuchukuliwa na maafisa wa polisi.

crime scene
crime scene

Mvulana wa miaka 15 ni mmoja wa washukiwa watatu waliokamatwa siku ya Jumapili kwa tuhuma za kuibia waendesha magari  katika barabara ya Southern Bypass.

Wakithibisha kukamatwa huko kupitia chapisho la Twitter, shirika la DCI limeripoti kuwa kijana huyo pamoja na wengine wawili , Brian Mwangi na Nickson Muchiri wenye umri wa miaka 25 kila mmoja walikamatwa kutokana na operesheni iliyofanywa na maafisa toka kituo cha Lang’ata.

Inadaiwa kuwa kijana huyo alikamatwa katika kichaka cha Ngong alipokuwa akijaribu kukwepa kukamatwa. Wawili wengine walikuwa wamekamatwa walipokuwa wanapanga njama ya kuibia waendesha magari.

Watatu hao walikuwa wamejihami na silaha aina ya panga waliyotumia kutishia na kuwaibia waathiriwa. Pikipiki mbili walizokuwa wakitumia kutekeleza uhalifu pia zilipatikana na kuchukuliwa na maafisa wale.

Waendesha wagari wanaotumia barabara hiyo wamekuwa wakilalamika kuvamiwa na vikundi za majambazi waliojihami  mara kwa mara.

Washukiwa 6 walikamatwa wiki iliyopita baada ya kuvamia mwendesha gari mmoja aliyekuwa anasafiri na mwanawe kutoka Nakuru kuelekea Nairobi akitumia bara bara hiyo hiyo. Tom Onyango alikuwa ameegesha gari ili kumruhusu mwanawe kuenda haja ndogo wakati walipovamiwa na kikundi cha majambazi sita waliokuwa wamejihami.