•Mwili wa Caroline ulivalishwa gauni la harusi kama alivyokuwa ameomba kupitia ujumbe wa simu.
•Marehemu pia alikuwa ameomba asizikwe nyumbani kwa aliyekuwa mumewe ila azikwe kwa wazazi wake Elgeyo Marakwet. Pale kijijini alikozikwa alijulikana sana kwa jina 'Chemu'
•Rekodi za shule ya msingi aliyosomea Caroline zinaashiria kuwa alikuwa mwanafunzi mwenye nidhamu na alihudumu kama kinara.
Hatimaye afisa mtoro Caroline Kangogo anayedaiwa kujitoa uhai kwa kujipiga risasi kichwani amezikwa nyumbani kwa wazazi wake katika kijiji cha Nyawa, kaunti ya Elgeyo Marakwet.
Mamia ya waombolezaji ikiwemo maafisa wa polisi zaidi ya 20 kutoka kituo cha polisi cha Nakuru alikokuwa anahudumu Bi Caroline walihudhuria hafla ya mazishi.
Hata hivyo, saluti 21 za bunduki hazikuwepo kama ilivyo desturi katika mazishi ya polisi yeyote aliyeaga nchini.
Mwili wa Caroline ulivalishwa gauni la harusi kama alivyokuwa ameomba kupitia ujumbe wa simu.
Marehemu pia alikuwa ameomba asizikwe nyumbani kwa aliyekuwa mumewe ila azikwe kwa wazazi wake Elgeyo Marakwet. Pale kijijini alikozikwa alijulikana sana kwa jina 'Chemu'
Rekodi za shule ya msingi aliyosomea Caroline zinaashiria kuwa alikuwa mwanafunzi mwenye nidhamu na alihudumu kama kinara.
Wanafamilia wengi hawakuamini kuwa 'Chemu' waliyejua ndiye alitekeleza mauaji ya wanaume wawili mapema mwezi huu.
Kakake marehemu, Mark Kangogo alisema kuwa dadake alikuwa mtu mzuri licha ya yale yaliandikwa kumhusu kwenye vyombo vya habari.
"Kama alitekeleza mauji yale kama ilivyoripotiwa basi ni vibaya. Hata niliuliza maafisa wakuu waliokuwa wanahudumu naye na walisema kuwa Caroline alikuwa afisa mzuri" Mark alisema.
Baadhi ya wanafamilia walidai kuwa hawakuwa wameridhishwa na upelelezi uliokuwa unaendelea na pia matokeo ya upasuaji wa mwili uliofanywa na mwapatholojia wa serikali Johansen Oduor.
Oduor alifanya upasuaji wa mwili wa Caroline mapema wiki hii ni kudai kuwa risasi ilimwingia marehemu kwenye upande wa kulia wa kichwa na kutokea upande wa kushoto.
Hata hivyo alidai kuwa uchunguzi zaidi ungefanywa kubaini kama kwamba alijipiga risasi mwenyewe ama alipigwa na mtu mwingine.
Kifo cha Caroline kiliibua mdahalo mkubwa nchini huku maswali yakiulizwa ikiwa alijitoa uhai ama aliuliwa na mwili wake kubebwa hadi bafuni alikopatikana ionekane kama kwamba alijitoa uhai mwenyewe.
Kunao baadhi ya wataalam waliotilia shaka ikawaje marehemu akajipiga risasi na kubaki na bastola aliyotumia mkononi.