Mwanafunzi amdunga kisu mpenziwe na kujaribu kujitoa uhai

Mshukiwa alikasirishwa na hatua ya mpenzi wake kutangaza kuwa anataka kumwacha.

Pingu
Image: Radio Jambo

Mwanafunzi alimdunga kisu mwenzake katika mzozo wa mapenzi kwenye Jengo la NHIF, Nairobi.

Mshukiwa ambaye ni mwanafunzi aliyekwenye mafunzo ya nyanjani katika ofisi moja iliyoko Jumba la NHIF alikasirishwa na hatua ya mpenzi wake kutangaza kuwa anataka kumwacha.

Mhasiriwa huyo ambaye ni mwanafunzi katika chuo kimoja huko Karen alikuwa amemletea kompyuta mpakato mshukiwa ofisini na kuiacha hapo kabla ya kumfuata kwenye lifti ambapo alimdunga kisu mara nne na baadaye kujaribu kujiua kwa kujikata koo.

Maafisa wa usalama waliwaokoa wawili hao na kuwakimbiza hospitalini ambapo walilazwa wakiwa katika hali mahututi.

Kwingineko,

Polisi wanachunguza kisa ambapo mwanamume mmoja alifikishwa katika hospitali moja eneo la Kasarani akiwa na majeraha ya kudungwa kisu na kufariki dakika chache baadaye.

Waendesha bodaboda wawili waliomleta mwathiriwa hospitalini walitoroka punde tu baada ya kumfikisha kumfikisha hospitalini.

 Walimweleza mhudumu katika hospitali ya Uhai Neema kwamba walimpata mwathiriwa kando ya barabara kuu ya Thika akiwa na majeraha ya kudungwa visu.

Muuguzi alipokuwa akimhudumia mwathiriwa, wawili hao walitoroka. Mwathiriwa alikufa dakika chache baadaye. Uchunguzi wa tukio hilo unaendelea.

Huku hayo yakijiri, Aliyekuwa mwakilishi wadi wa Marungu huko Taita Taveta Paul Waweru siku Jumanne alifikishwa katika mahakama moja mjini Voi akikabiliwa na tuhuma za kuharibu mnara wa stima wenye thamani ya shilingi millioni 8 na kumiliki vifaa vya wizi mali ya  kampuni ya umeme ya Kenya Power.

Afisa mkuu anayesimamia kitengo cha usalama katika kampuni hiyo kanda ya Pwani meja staafu Antony Mganda aliambia mahakama kuwa Waweru ni mmoja wa washukiwa wanaoshukiwa kujihusisha na uharibifu wa vifaa vya Kenya Power.

Aliachiliwa kwa dhamana ya shilingi millioni tatu huku kesi hiyo ikiratibiwa kutajwa tarehe 4 oktoba.