Rais Ruto awaomboleza maafisa wa KDF waliofariki katika ajali ya helikopta Lamu

"Dua zetu ziko kwa Wanajeshi wa Ulinzi wa Kenya na wale wote ambao wameathiriwa na mkasa huo."

Muhtasari
  • KDF ilisema katika taarifa kwamba ndege hiyo ilianguka Jumatatu usiku wakati wa uchunguzi wa anga kwa Operesheni inayoendelea Amani Boni, na kuua idadi isiyojulikana ya wafanyikazi.
Rais Ruto kuongeza idadi ya watoza ushuru kwenye masoko, mitaa.
Rais Ruto kuongeza idadi ya watoza ushuru kwenye masoko, mitaa.
Image: Facebook

Rais William Ruto ametuma risala za rambirambi kwa familia za maafisa wa jeshi walioangamia baada ya helikopta ya Kenya Airforce Huey kuanguka katika kaunti ya Lamu.

KDF ilisema katika taarifa kwamba ndege hiyo ilianguka Jumatatu usiku wakati wa uchunguzi wa anga kwa Operesheni inayoendelea Amani Boni, na kuua idadi isiyojulikana ya wafanyikazi.

"Rambirambi zetu kwa familia na marafiki kwa msiba wa mashujaa wetu katika ajali ya helikopta Lamu. Tunaheshimu ushujaa wao katika kutetea na kulinda mamlaka ya Kenya," Ruto alisema katika taarifa Jumanne jioni.

"Dua zetu ziko kwa Wanajeshi wa Ulinzi wa Kenya na wale wote ambao wameathiriwa na mkasa huo."

KDF ilisema katika taarifa kwamba bodi ya uchunguzi imeundwa na kutumwa katika eneo la tukio ili kubaini chanzo cha ajali hiyo.

"Uongozi na udugu wote wa KDF unawapa pole familia za wafanyakazi," Mkuu wa Mawasiliano ya Kijeshi wa KDF Brigedia Zipporah Kioko alisema lakini hakufichua idadi ya maafisa waliofariki katika ajali hiyo.