Kamati ya Seneti inayochunguza vifo vya Shakahola yatembelea Kanisa la Ezekiel

Mnamo Ijumaa, mhubiri Ezekiel Odero aliwakaribisha wanakamati ya Seneti katika Kanisa lake.

Muhtasari

•Kamati hiyo ilitua kwenye uwanja wa ndege wa Mombasa mwendo wa saa mbili unusu asubuhi na wakaelekea moja kwa moja hadi Mavueni.

mchungaji Ezekiel Odero
mchungaji Ezekiel Odero
Image: Facebook

Kamati ya Seneti inayochunguza vifo vya Shakahola imetembelea Kanisa la  New life Prayer Center inayoogozwa na Mchungaji Ezekiel Odero.

 Kamati hii ya muda yenye maseneta  11 inayoongozwa na Seneta wa Tana River, Danson Mungatana ilitua kwenye uwanja wa ndege wa Mombasa mwendo wa saa mbili unusu asubuhi na wakaelekea moja kwa moja hadi Mavueni, ambako ni makao makuu ya kanisa hilo.

Ezekiel Odero siku chache zilizopita alifanyiwa mahojiano ya moja kwa moja na kamati ya seneti ili kujibu mahusiano yake na mchungaji mwenye utata Paul Mackenzie wa Kanisa la Good News International.

Mchungaji huyu aliwaomba maseneta kuzuru kanisa lake  lililoko Mavueni kaunti ya Kilifi  ili kufanya uchunguzi wao  jinsi shughuli za maombi zinafanyika katika kanisa hilo

Wakati wa mahojiano ya moja kwa moja katika seneti , Ezekiel alikiri kutokuwa na uhusiano wowote na mchungaji mwenye utata Paul MacKenzie ambaye alidaiwa kusababisha vifo zaidi ya mia nne kupitia kile kilichodaiwa kuwashirikisha wafuasi wake katika mfungo wa imani .

Ezekiel alielezea seneti kuwa kanisa lake lina zaidi ya washirika 45,000. Mchungaji huyo alitakiwa kueleza jinsi alivyomiliki zaidi ya Akaunti tano za benki .

"Washirika wangu wanapotoa sadaka sisi kama kanisa la Newlife tunafanya kikao na wakuu wa kanisa ili tuweze kujadiliana  jinsi ambavyo tutasaidia wakazi wa Kilifi  kupitia ajira mfano tumefungua Hoteli ambayo ni ajira kwa wengi," alisema mchungaji huyo.