Watu 2 waaga baada ya mlipuko katika kiwanda cha gesi Embakasi

Takriban waathiriwa 167 wametibiwa katika hospitali ya Mama Lucy jijini Nairobi.

Muhtasari

• Mlipuko huo ulitokea karibu usiku wa manane na video zilizochapishwa kwenye mitandao ya kijamii zilionyesha moto mkubwa ukiwaka karibu na nyumba za ghorofa.

Picha za eneo la mlipuko wa gesi huko Embakasi, Nairobi. Picha: SCREENGRAB
Picha za eneo la mlipuko wa gesi huko Embakasi, Nairobi. Picha: SCREENGRAB

Watu wasiopungua wawili waliuawa baada ya mlipuko katika kiwanda cha gesi eneo la Embakasi, Nairobi.

Mkuu wa polisi wa Embakasi Wesley Kimeto alithibitisha waliofariki wakiwa mtu mzima mmoja na mtoto mdogo, kufikia saa kumi na nusu asubuhi.

Alisema huenda idadi hiyo ikaongezeka.

Mlipuko huo ulitokea karibu usiku wa manane na video zilizochapishwa kwenye mitandao ya kijamii zilionyesha moto mkubwa ukiwaka karibu na nyumba za ghorofa.

Shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya lilisema hatua za pamoja za vitengo mbalimbali vya kukabiliana na majanga zilifanikisha kuhamishwa kwa watu 271 hadi vituo tofauti vya afya jijini Nairobi.

Kufikia sasa, takriban waathiriwa 167 wametibiwa katika hospitali ya Mama Lucy jijini Nairobi. Hii inajumuisha watu wazima 142 na watoto 25, wengi wakiwa na majeraha ya kuvuta moshi.

Takriban saba kati ya waathiriwa waliojeruhiwa vibaya walihamishiwa Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH) na wengine 17 katika hospitali ya Chuo Kikuu cha Kenyatta.

Wagonjwa kadhaa walitibiwa na kuruhusiwa kurudi makwao.

Kufikia saa 12:30 asubuhi siku ya Ijumaa, polisi wa Embakasi walisema moto umedhibitiwa na sasa wanapitia miundo ili kuangalia kama kuna majeruhi zaidi.

"Inaweza kuchukua muda lakini tuna wataalam wa kupekua mabaki kuona kuna wahasiriwa," alisema.

Msemaji wa serikali Isaac Mwaura alisema mitungi ya gesi ilikuwa ikijazwa moto huo ulipozuka kabla ya saa sita usiku Alhamisi.

Chanzo cha moto huo bado hakijabainika, Mwaura alisema.

Wazima moto na wahudumu wa dharura wapo katika eneo ambalo kampuni ya Kentainers Company Ltd iko, kulingana na polisi.

Walioshuhudia walisema walihisi tetemeko mara baada ya mlipuko huo.

Shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya lilisema kwenye mitandao ya kijamii kuwa wafanyakazi wamekuwa "wakipambana na moto" na kusema kuwa watu 29 wamepelekwa hospitalini wakiwa na majeraha.

Moto huo ulisambaa katika majengo kadhaa ya ghorofa, na kusababisha hofu kwamba idadi ya waliopoteza maisha inaweza kuongezeka zaidi.

Imetafsiriwa na Davis Ojiambo.