logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Makamu wa Rais wa Malawi afariki dunia katika ajali ya ndege

Saulos na wengine 9 walikuwa wakisafiri Jumatatu wakati ndege yao ilipotoweka.

image
na Davis Ojiambo

Habari11 June 2024 - 15:05

Muhtasari


  • • Makamu wa rais na rais wanatoka vyama tofauti lakini wawili hao waliungana kuunda muungano wakati wa uchaguzi wa 2020.
Marehemu Makamu wa Rais wa Malawi Dkt. Saulos Chilima, alifariki katika ajali ya ndege.

Mabaki ya ndege iliyombeba makamu wa rais wa Malawi imepatikana bila mtu yeyote aliyenusurika, Rais Lazarus Chakwera amesema.

Saulos Chilima na wengine tisa walikuwa wakisafiri nchini humo Jumatatu asubuhi wakati ndege yao ilipotoweka kwenye rada za uwanja wa ndege.

Ndege hiyo kijeshi, ilikuwa ikisafiri hali mbaya ya hewa.

Wanajeshi walikuwa wakipekua Msitu wa Chikangawa katika juhudi za kuitafuta ndege hiyo.

Katika kikao na wanahabari siku ya Jumanne, Rais Chakwera alisema kamanda wa Jeshi la Ulinzi la Malawi alimweleza kuwa shughuli ya utafutaji na uokoaji imekamilika na ndege hiyo kupatikana.

Bw Chakwera alisema "alihuzunishwa na kusikitika sana" kuwafahamisha Wamalawi kuhusu mkasa huo mbaya.

Alisema timu ya uokoaji ilikuta ndege hiyo ikiwa imeharibika kabisa.

Makamu wa rais na rais wanatoka vyama tofauti lakini wawili hao waliungana kuunda muungano wakati wa uchaguzi wa 2020.

Dk Chilima (51) alikuwa akielekea kuiwakilisha serikali katika mazishi ya aliyekuwa waziri wa serikali Ralph Kasambara aliyefariki siku nne zilizopita.

Mke wa Rais wa zamani Shanil Dzimbiri pia alikuwa kwenye ndege hiyo, iliyopaa kutoka mji mkuu, Lilongwe, Jumatatu asubuhi.

Ilikusudiwa kutua kwenye uwanja wa ndege katika mji wa kaskazini wa Mzuzu, lakini ilirudishwa kwa sababu ya hali mbaya ya hewa .

Dk Chilima amekuwa makamu wa rais wa Malawi tangu 2014.

Alipendwa sana nchini Malawi, hasa miongoni mwa vijana, shirika la habari la AFP linaripoti.

Hata hivyo, Dk Chilima alikamatwa na kufunguliwa mashtaka mwaka 2022 kwa madai kwamba alikubali pesa ili kutoa kandarasi za serikali.

Mwezi uliopita, mahakama ilitupilia mbali mashtaka hayo, bila kutoa sababu za uamuzi huo.

Dk Chilima ameoa na ana watoto wawili.

Saulos Chilima ni nani?

  • Kabla ya taaluma yake ya kisiasa, alishikilia nyadhifa muhimu za uongozi katika kampuni za kimataifa kama Unilever na Coca Cola.
  • Bw Chilima, mwenye umri wa miaka 51, amekuwa makamu wa rais wa nchi hiyo ya kusini mwa Afrika tangu 2014.
  • Ameoa na ana watoto wawili.
  • Dk Chilima anatajwa kwenye tovuti ya serikali kuwa ni "mtendaji", "mchapa kazi" na "mfanisi"
  • Ana PhD katika Usimamizi wa Maarifa

RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved