Vijana waandamana dhidi ya mswada wa fedha 2024 siku ya pili

Maandamano hayo yameshuhudiwa Nairobi, Mombasa, Kisumu, Kisii, Nakuru, Nyeri na Eldoret

Muhtasari

•Mrengo wa upinzani wa Azimio Kenya One umeunga mkono maandamano ya vijana machachari ya kizazi kipya cha Gen Z ambayo hayajaegemea mrengo wowote wa kisiasa.

•Baadhi ya wabunge akiwemo Owen Baya, mbunge wa Kilifi Kaskazini, wamejitokeza na kusema kuwa maandamano hayo yamefadhiliwa na kundi la fulani la watu ambalo hakutaja

•“Sisi ndisi Raila mpya, sisi ndisi James Orengo mpya. Naam! Mlizoea kusema kuwa maandamano yalikuwa yanaandaliwa na Raila Odinga na timu ya ODM na wapinzani wa serikali.

•Maandamano hayo yamezidi kupamba moto nchini huku yakishuhudiwa Nairobi, Eldoret, Kisii, Kisumu, Nyeri na Mombasa.

Wakenya waandamana dhidi ya Mswada wa Fedha 2024
Image: BBC

Macho yote yameelekezwa kwenye bunge hii leo huku Mswada wa Fedha wa mwaka 2024 ukizidi kuzua mzozo na patashika miongoni mwa wakenya.

Hata hivyo, maandamano yamezidi kuchacha kila uchao katika sehemu mbalimbali za nchi ikiwemo hii leo ambapo yanatarajiwa kuingia siku ya pili jijini Nairobi baada ya awamu ya kwanza iliyofanyika mnamo Jumanne wiki hii.

Mrengo wa upinzani wa Azimio Kenya One umeunga mkono maandamano ya vijana machachari ya kizazi kipya cha Gen Z ambayo hayajaegemea mrengo wowote wa kisiasa.

Hata hivyo, baadhi ya wabunge akiwemo Owen Baya, mbunge wa Kilifi Kaskazini, wamejitokeza na kusema kuwa maandamano hayo yamefadhiliwa na kundi la fulani la watu ambalo hakutaja.

“Hiki ni kitu ambacho kimepangwa na wameona kundi ambalo ni rahisi kushawishi ni Gen Z. Wameona kundi ambalo ni rahisi kwa kusukuma ajenda zetu ni Gen Z,” alisema mbunge Baya ambaye alikuwa msiri kutaja waliohusika katika kudhamini maanadamano hayo.

“Sisi ndisi Raila mpya, sisi ndisi James Orengo mpya. Naam! Mlizoea kusema kuwa maandamano yalikuwa yanaandaliwa na Raila Odinga na timu ya ODM na wapinzani wa serikali lakini mnaona memba yeyote wa ODM? Hamna yeyote ambaye amevaa shati ya Wiper na Jubilee hapa sisi ni wakenya, wakenya wa kawaida ambao wamechoka nah ii serikali,” alisema kijana mmoja akizungumzana KTN ambaye jina lake hakusema.

Maandamano hayo yamezidi kupamba moto nchini huku yakishuhudiwa maeneo ya Nairobi, Eldoret, Kisii, Kisumu, Nakuru, Nyeri na Mombasa. Kando na hayo,vilevile yameshuhudiwa mtandaoni ambapo ndiyo nguzo na uti wa mgongo wa maandamano hayo kwani humo ndimo yalianzia.

Aidha, hali si hali tena kwani maandamano hayo yamezidi kuvuma si nchini tu bali hata nje ya nchi. Nchini Qatar, kizazi cha Gen Z cha Kenya kilikuwa kinavuma kwenye mtandao wa kijamii wa X na kauli mbiu ikiwa #reject the finance bill.

Maandamano hayo yameshuhudia askari wakidhulumu haki za wananchi na uhuru wa kuandamana kwani wapo baadhi ya wananchi ambao wamepelekwa korokoroni kwa kuandamana kwa utulivu na amani kwa mujibu wa kipengee cha 37 cha katiba ya Kenya.