Wajane wa waliokuwa maafisa wa KDF wataka sera ya pensheni kubadilishwa

Wajane hao wanasema muda wa sasa wa miaka 5 ni mfupi sana na mdogo ikilinganishwa na huduma inayotolewa na wenzi wao.

Muhtasari

• Maafisa wastaafu wa KDF chini ya mwavuli wa Kenya Veterans for peace siku ya  Jumatano walitoa misaada kwa wenzao waliostaafu na familia zao.

Maafisa wastaafu wa KDF chini ya mwavuli wa Kenya Veterans for peace siku ya Jumatano walitoa misaada kwa wenzao waliostaafu na familia za maafisa walioaga katika kaunti ya Kisumu.
Maafisa wastaafu wa KDF chini ya mwavuli wa Kenya Veterans for peace siku ya Jumatano walitoa misaada kwa wenzao waliostaafu na familia za maafisa walioaga katika kaunti ya Kisumu.
Image: HISANI

Wajane wa maafisa waliostaafu wa Jeshi la Ulinzi la Kenya KDF wanaitaka serikali kufanyia marekebisho muda wa miaka mitano wanaopokea pensheni ya waume zao wanapofariki.

Wajane hao wanasema muda wa sasa wa miaka 5 ni mfupi sana na mdogo ikilinganishwa na huduma inayotolewa na wenzi wao.

"Serikali inapaswa kuangalia pensheni ya maafisa wastaafu wa KDF, mume wangu alikufa miaka miwili baada ya kustaafu hakufurahiya hata kustaafu kwake na mimi nilipewa pensheni yake kwa miaka mitano tu, hiyo ilikuwa fupi sana na serikali inahitaji kufanya kitu”, Alisema mjane Victoria Okello.

 Maafisa wastaafu wa Jeshi la Ulinzi la Kenya chini ya mwavuli wa Kenya Veterans for peace siku ya  Jumatano walitoa misaada kwa wenzao waliostaafu na familia za maafisa walioaga kutoka kaunti ya Kisumu.

Walisambaza vyakula vya aina mbalimbali kwa familia 150 ili kuzisaidia katika nyakati hizi ngumu za kiuchumi.

Image: HISANI

Nelson Sechere, mkurugenzi mtendaji wa Kenya Veterans for Peace, alisema wanalenga kaunti zote na pia wanachimba visima kadhaa ili kuchangia usalama wa chakula nchini.

"Kazi yetu ni kuwashukuru maafisa wa zamani wa KDF ambao wanaishi katika maisha ya kusikitisha, hayaendelezi hadhi ya afisa wa kijeshi", alisema mkurugenzi mtendaji Nelson Sechere.

Mwaka 2022 Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta alitia saini kuwa sheria Mswada wa Mashujaa wa Kijeshi, 2022.

Sheria, ambayo inaweka mfumo wa udhibiti na kitaasisi kwa ajili ya usimamizi wa masuala ya mashujaa wa kijeshi, inatoa manufaa kwa maafisa waliostaafu au kufariki na wategemezi wao ikiwa ni pamoja na kuanzishwa kwa Hazina ya Elimu ya Wategemezi kupitia Baraza la Ulinzi.

Hazina hiyo inatoa ufadhili wa masomo kwa ajili ya elimu ya mayatima wa waliokuwa maafisa wa kijeshi. Sheria hiyo pia inatoa masharti kwa Baraza la Ulinzi kuagiza kanuni za usimamizi wa Hazina ikiwa ni pamoja na utaratibu wa kushughulikia maombi ya ufadhili wa masomo.