Hatma ya gavana Mwangaza mikononi mwa Njuri Ncheke

Rais William Ruto na viongozi wengine wakuu wa Chama cha UDA walikuwa wamewaomba wanasiasa wa Meru kumaliza migogoro ya kisiasa inayojirudia

Muhtasari

•Rais William Ruto alitoa maelekezo kuhusu suala hili na kuagiza MCA na gavana kutafuta njia mbadala ya kutatua mizozo na kuepuka njia ya kuondoa madaraka.

•Gavana wa Meru aliiambia mahakama kwamba hoja hiyo ilitokana na chuki kutoka kwa wapinzani wake wa kisiasa.

GAVANA WA MERU KAWIRA MWANGAZA
Image: EZEKIEL AMING'A

Mahakama Kuu ya Kenya iliamua siku ya Jumatatu, Julai 29, kwamba hoja ya kumuondoa madarakani Gavana wa Meru, Kawira Mwangaza, itarejeshwa kwa Baraza la Wazee la Njuri Njeke.

Wajumbe wa Bunge la Kaunti (MCA) walikuwa wamewasilisha hoja ya nne ya kummg'oa gavana madarakani.

Rais William Ruto alitoa maelekezo kuhusu suala hili na kuagiza MCA na gavana kutafuta njia mbadala ya kutatua mizozo na kuepuka njia ya kuondoa madaraka.

“Baraza la Wazee wa Njuri Njeke la Wameru linaagizwa kuwasilisha maamuzi yao au ukosefu wake kuhusu mzozo kati ya pande hizi kama ilivyoelekezwa na Rais wa Jamhuri ya Kenya, isipite zaidi ya wiki tatu kutoka leo,” ilisema amri ya Mahakama Kuu ya Meru.

“Pande hizi zinagizwa kujitokeza mbele ya NJURI NJEKE na mawakili wao kabla ya Jumatano, Julai 31, 2024.”

Mahakama Kuu ilitaja kwamba kama njia ya kukuza utatuzi wa mizozo kwa njia mbadala, kama alivyoelekeza Kiongozi wa Nchi, hakuna hukumu itakayotoa kuhusu hoja ya kumvua madaraka gavana kwa wakati huu.

“Jua kwamba kutokuzingatia au kutotekeleza amri ya mahakama iliyotolewa hapa kutasababisha adhabu kwa wewe na mtu mwingine yeyote anayekiuka na kutotekeleza amri hiyo,” sehemu ya hukumu ilisema.

Kawira Mwangaza alikuwa ameenda kortini tarehe 24 Julai, kutafuta amri ya kuzuia MCA kuendelea na hoja ya nne ya kumvua madaraka.

Gavana wa Meru aliiambia mahakama kwamba hoja hiyo ilitokana na chuki kutoka kwa wapinzani wake wa kisiasa.

Aliongeza kwamba wapinzani wake walikuwa wamepiga sahihi za MCA waliomuunga mkono kwa ajili ya kufikia kigezo cha kujadili hoja ya kumvua madaraka.

Rais William Ruto na viongozi wengine wakuu wa Chama cha United Democratic Alliance (UDA) walikuwa wamewaomba wanasiasa wa Meru kumaliza migogoro ya kisiasa inayojirudia.

Ingawa alichaguliwa kama mgombea huru, Kawira Mwangaza alijiunga na UDA mnamo Aprili 3, ambayo ndiyo chama kinachotawala katika Bunge la Kaunti ya Meru.