'Igwee igwee', Kaimu Katibu mkuu wa UDA apokelewa kwa vigelegele

Kulikuwa na maafisa wengi wa polisi baada ya uteuzi wa Cleophas Malala kubatilishwa.

Muhtasari

• Mkutano huo wa NEC uliongozwa na mwenyekiti wa chama hicho na Gavana wa Embu Cecily Mbarire.

• Malala aliteuliwa kuwa Kaimu Katibu Mkuu wa UDA Februari 2023.

• Siku ya Jumanne, wakili Joe Khalende alivamia makao makuu ya chama cha UDA akidai kuchukua nafasi ya Katibu Mkuu.

Wakiwa wamebeba matawi ya miti, wafuasi wa Omar waliimba nyimbo za kuunga mkono kaimu katibu mkuu mpya.

"SG, SG... Igwee igwee," walishangilia.

Mapema Ijumaa, kulikuwa na maafisa wengi wa polisi baada ya uteuzi wa Cleophas Malala kubatilishwa.

Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama cha UDA ilitengua uteuzi wa Katibu Mkuu Cleophas Malala na nafasi yake kuchukuliwa na Omar.

“Baada ya majadiliano mapana na ya mashauriano, kwa kuzingatia na kwa mujibu wa mamlaka yake chini ya Ibara ya 8.2 ya Katiba ya Chama, Halmashauri Kuu ya Taifa imeazimia kumteua Makamu Mwenyekiti, Mheshimiwa Hassan Omar Hassan kukaimu nafasi ya Katibu Mkuu. Kwa muda," taarifa ilisema.

Mkutano huo wa NEC uliongozwa na mwenyekiti wa chama hicho na Gavana wa Embu Cecily Mbarire.

Malala aliteuliwa kuwa Kaimu Katibu Mkuu wa UDA Februari 2023. Alichukua nafasi ya Veronica Maina ambaye aliteuliwa katika Seneti.

Chama tawala cha UDA katika siku za hivi majuzi kimekuwa na malumbano ya ndani kwa ndani kuhusu nafasi hiyo.

Baadhi ya wanachama wa UDA wamekuwa wakitaka Malala aondolewe.

Siku ya Jumanne, wakili Joe Khalende alivamia makao makuu ya chama cha UDA akidai kuchukua nafasi ya Katibu Mkuu.

Khalende pia alidai kuwa Malala amekuwa hachukulii majukumu yake kama SG kwa uzito hivyo kuwepo haja ya kuchukua nafasi yake.

"Anapinga uundwaji wa serikali pana na niko hapa kuthibitisha kuwa yeye si Katibu Mkuu tena wa chama cha UDA.

Mimi Joe Khalende nitachukua nafasi ya Katibu Mkuu wa chama cha UDA," alisema.

"Kwa mbele, chama cha UDA kinarejea kwa wanachama wake. Kilianzishwa kama chama kinachozingatia watu, sio watu binafsi ndani ya chama."

Mwenyekiti Mbarire, hata hivyo, alipuuzilia mbali madai ya Khalende akisema kuwa UDA ni chama ambacho kina miundo inayoongoza shughuli zake.

Kaimu Katibu Mkuu wa Chama cha United Democratic Alliance (UDA) Hassan Omar amepokelewa kwa shangwe na ngoma katika Makao Makuu ya Chama.

IMETAFSIRIWA NA DAVIS OJIAMBO.