logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Gavana Waiguru ataka asasi za usalama kuhakikisha mshukiwa wa unyanyasaji wa kijinsia kaunti ya Nakuru anakamatwa

Mshukiwa wa unyanyasaji wa kijinsia katika kaunti ya Nakuru ni mhubiri wa kanisa moja eneo hilo

image
na Brandon Asiema

Yanayojiri22 November 2024 - 16:25

Muhtasari


  • Mwathiriwa anaendelea kupata matibabu katika hospitali moja kwenye kaunti hiyo chini ya uangalizi mkali kutokana na hofu ya wanafamilia wake kuhofia kuwa anaweza kushambuliwa tena.
  • Gavana Waiguru amekashifu tukio hilo la mapema wiki hii akisema kuwa kuna njia mwafaka za kusuluhisha mizozano ya kinyumbani bila ya vurugu akisisitiza kuwa ukatili wa kijinsia hauna nafasi katika jamii.

caption

Gavana wa kaunti ya Kirinyaga Anne Waiguru amekuwa kiongozi wa hivi punde kushinikiza asasi za usalama kuhakikisha kuwa mshukiwa wa unyanyasaji wa kiijinsia katika kaunti ya Nakuru anakamatwa na kufikishwa mahakani ili haki ipatikane kwa kitendo cha unyama alichotekeleza.

Kupitia ukurasa wake wa X, gavana Waiguru amekashifu tukio hilo akisema kuwa kuna njia mwafaka za kusuluhisha mizozano ya kinyumbani bila ya vurugu akisisitiza kuwa ukatili wa kijinsia hauna nafasi katika jamii.

“Nalaani kisa cha kusikitisha huko Nakuru, ambapo mwanamume alimvamia mkwewe katika mzozo wa kinyumbani. Kwa vyovyote vilekatika kutokubaliana, hatupaswi kamwe kutumia vurugu. Ukatili wa kijinsia hauna nafasi katika jamii yetu.” Alisema gavana Anne Waiguru.

Mshukiwa ambaye ni mhubiri katika kanisa moja jijini Nakuru, anadaiwa kutekeleza kisa ambapo alimvamia mkewe kwa silaha yenye makali na kumwacha na majeraha makali kabla ya kutoroka.

Inaarifiwa kuwa mshukiwa alijaribu kuwavamia wanawe wawili wenye umri wa miaka miwili na kumi kabla ya majirani kuingilia kati na kuwaokoa.

Akidhibitisha kisa hicho, afisa mkuu wa jinsia katika kaunti ya Nakuru Gladys Kamuren, aliwataka wakaazi kuwa na utulivu uchunguzi unapoendelezwa na polisi wa kumkamata mshukiwa.

Mwathiriwa anaendelea kupata matibabu katika hospitali moja kwenye kaunti hiyo chini ya uangalizi mkali kutokana na hofu ya wanafamilia wake kuhofia kuwa anaweza kushambuliwa tena.

Ukatili wa mhubiri huyo kwa mke wake unajiri saa chache baada ya rais William Ruto kukashifu visa vya wanawake kuuliwa nchini huku akitenga shilingi milioni mia moja kuendesha kampeni ya kuhamasisha wananchi dhidi ya ukatili kwa wanawake.

Katika miezi  michache ya hapo nyuma, idadi ya mauaji dhidi ya wanawake iliripotiwa kukithiri, data za utafiti zikionyesha kuwa angalau wanawake 97 waliuliwa ndani ya miezi mitatu pekee.



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved