logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Washukiwa Wa Ugaidi Wakamatwa Mandera Wakipanga Kuwateka Nyara Raia Wa Kigeni

Mshukiwa mkuu anadaiwa kuingia nchini kutoka El-Ade, Somalia, na kutengeneza stakabadhi ghushi ili ajitambulishe kama Mkenya.

image
na Samuel Mainajournalist

Yanayojiri18 February 2025 - 09:30

Muhtasari


  • Washukiwa wanaripotiwa kupanga utekaji nyara wa raia wa kigeni waliokuwa wakifanya kazi kwenye mradi wa ujenzi wa mtaro wa maji.
  • Uchunguzi wa kina ulibaini kuwa mshukiwa huyo alikuwa ameandaa malipo ya KSh 100,000 kwa mshirika wake wa hapa nchini.
Crime scene

Polisi wa kupambana na ugaidi mnamo Jumanne asubuhi waliwakamata washukiwa wawili wa kundi la Al Shabaab katika kaunti ya Mandera.

Wawili hao wanaripotiwa kuwa walikuwa wakipanga utekaji nyara wa raia wa kigeni waliokuwa wakifanya kazi kwenye mradi wa ujenzi wa mtaro wa maji taka katika mji wa Mandera.

 Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), msako wa kiintelijensia uliongoza maafisa wa usalama kumkamata mshukiwa mkuu, Isaac Abdi Mohamed, anayejulikana pia kama Kharan Abdi Hassan, mwenye umri wa miaka 29.

 Inadaiwa kuwa alijipenyeza nchini hivi majuzi kutoka El-Ade, Somalia, na kutengeneza stakabadhi ghushi ili ajitambulishe kama Mkenya.

 Uchunguzi wa kina ulibaini kuwa mshukiwa huyo alikuwa ameandaa malipo ya KSh 100,000 kwa mshirika wake wa hapa nchini, ambaye angehusika katika utekelezaji wa utekaji nyara huo.

 Aidha, iligunduliwa kuwa washukiwa walipanga kuwahamisha waathiriwa hadi El-Ade kwa gharama ya KSh 300,000, kwa usaidizi wa mshirika wake wa pili, Noor Yacob Ali, mwenye umri wa miaka 29.

 Katika operesheni nyingine iliyofanyika mapema leo, vikosi vya usalama vya pamoja vilifanikiwa kumnasa Yacob Ali katika eneo la Metameta, ndani ya Mandera township.

 Kwa sasa, washukiwa hao wanazuiliwa na wanaendelea kuhojiwa kabla ya kufikishwa mahakamani kwa mashitaka ya kuwa wanachama wa kundi la kigaidi, kosa linaloangukia chini ya Sheria ya Kuzuia Ugaidi (POTA).

 Maafisa wa usalama wamewataka wananchi kushirikiana na vyombo vya usalama kwa kutoa taarifa za kutiliwa shaka ili kuhakikisha usalama unadumishwa.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved