logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Kenya yaibuka bora barani Afrika kwenye mashindano ya Olimpiki yaliyotamatika Tokyo

Hatimaye mashindano ya Olimpiki yaliyokuwa yanafanyika jijini Tokyo, Japan yalitamatika siku ya Jumapili baada ya siku 17

image
na Radio Jambo

Yanayojiri09 August 2021 - 02:59

Muhtasari


•Ushindani mkali ulishuhudiwa kwenye mashindano hayo huku Marekani ikiibuka mshindi  baada ya kunyakua medali 113

•Kenya iliweza kuondoka pale na medali 10; nne zikiwa za dhahabu, nne za fedha na mbilli za shaba

Eliud Kipchoge baada ya kushinda dhahabu usiku wa kuamkia Jumapili

Hatimaye mashindano ya Olimpiki yaliyokuwa yanafanyika jijini Tokyo, Japan yalitamatika siku ya Jumapili baada ya siku 17.

Ushindani mkali ulishuhudiwa kwenye mashindano hayo huku Marekani ikiibuka mshindi  baada ya kunyakua medali 113. China na Japan zilishikilia nafasi ya pili na ya tatu zikijinyakulia medali 88 na 58 mtawalia. 

Hata hivyo mataifa ya bara Afrika yalishindwa kung'aa kwenye mashindano hayo huku ushindi wa Eliud Kipchoge usiku wa kuamkia Jumapili ukisukuma Kenya katika nafasi ya 19 kote duniani na kileleni miongoni mwa mataifa ya bara Afrika.

Kenya iliweza kuondoka pale na medali 10; nne zikiwa za dhahabu, nne za fedha na mbilli za shaba. Nchi jirani ya Uganda ilishikilia nafasi ya 35 kote duniani na kuibuka wa pili barani Afrika baada ya kujinyakulia dhahabu mbili, fedha moja na medali moja ya shaba.

Afrika Kusini ilishikilia nafasi ya tatu barani ikienda nyumbani na dhahabu moja na fedha mbili. Taifa la Misri lilijinyakulia dhahabu moja, fedha moja  na nishani nne za shaba. Ethiopia ilifunga orodha ya tano bora barani Afrika na nishani moja ya dhahabu, fedha moja na shaba mbili.

Medali nne za dhahabu ambazo  Kenya ilinyakua zilitwaliwa na Emmanuel Korir, Peres Jepchirchir, Faith Kipyegon na Eliud Kipchoge.

 Ferguson Rotich, Brigid Kosgei, Timothy Cheruiyot  na Hellen Obiri walinyakulia Kenya nishani za fedha huku  Benjamin Kigen na Hyvin Kiyeng wakishinda shaba.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved