logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Kipa wa Barcelona, Ter Stegen, ajibu madai ya redio kuwa ndoa yake ilivunjika kufuatia usaliti wa mkewe

Ter Stegen amesisitiza kuwa hakukuwa na usaliti wowote katika ndoa yake ya miaka minane.

image
na Samuel Mainajournalist

Football11 March 2025 - 08:24

Muhtasari


  • Ter Stegen alithibitisha rasmi kuwa ndoa yao ilikuwa imevunjika, ingawa alisisitiza kuwa walitengana kwa amani.
  •  Stegen aliwashutumu waandishi wa habari Juliana Canet, Roger Carandell na Marta Montaner kwa kueneza uvumi usio na msingi.

Marc ter stegen na aliyekuwa mkewe Daniela Jehle

Kipa wa FC Barcelona, Marc-André ter Stegen, ameibuka hadharani kukemea vikali kituo cha redio cha Catalunya Radio na kampuni ya 3Cat Group kwa kusambaza taarifa za uongo kuhusu sababu ya kutengana kwake na mkewe wa zamani, Daniela Jehle.

Katika taarifa rasmi aliyotoa siku ya Jumatatu, Machi 10, Ter Stegen alikanusha madai kuwa ndoa yake ilivunjika kutokana na usaliti wa Daniela, akiwashutumu waandishi wa habari Juliana Canet, Roger Carandell na Marta Montaner kwa kueneza uvumi usio na msingi.

"Nimeshtushwa na kusikitishwa na usimamizi mbovu na ukosefu wa uongozi katika Catalunya Radio na 3Cat Group – vyombo vinavyosambaza habari za uongo na kukiuka haki za kibinafsi," aliandika kipa huyo.

Kwa mujibu wa taarifa yake, Ter Stegen alisisitiza kuwa hakukuwa na usaliti wowote katika ndoa yake, wala mtu wa tatu aliyehusika katika uamuzi wao wa kutengana.

"Hakujawa na usaliti wowote kutoka kwa Daniela. Hakuna mtu mwingine aliyehusika. Huu ni ukweli," alisisitiza.

Hata hivyo, alieleza kuwa yeye na Daniela walifikia makubaliano ya kutengana kwa hali ya amani na maelewano mazuri, wakibaki na mawasiliano yenye heshima.

Kipa huyo raia wa Ujerumani alionyesha ghadhabu kwa jinsi taarifa za uongo zilivyomchafulia mke wake wa zamani hadharani, akielezea kusikitishwa kwake na ukweli kuwa chombo kikuu cha habari kinachomilikiwa na serikali kimekuwa sehemu ya kusambaza uvumi huo.

"Ni jambo lisilokubalika hata kidogo kwa shirika kubwa la habari linalomilikiwa na serikali kusambaza habari hizi zisizo na msingi, ambapo Daniela anatuhumiwa kwa uwongo na kushambuliwa binafsi," aliongeza.

Mlinda lango huyo alihitimisha kwa kusema kuwa uharibifu uliosababishwa na uvumi huo hauwezi kurekebishwa.

"Madhara yaliyosababishwa hayawezi kurekebishwa. Asanteni," alisema.

Ter Stegen na Daniela walikuwa kwenye mahusiano kwa muda mrefu kabla ya kuoana mnamo mwaka wa 2017.

Daniela, ambaye ni mbunifu wa usanifu wa majengo, alikuwa akiishi pamoja na kipa huyo jijini Barcelona, na mara kwa mara walionekana pamoja kwenye matukio ya kijamii na mechi muhimu za Blaugrana.

Hata hivyo, mnamo Februari 2024, ripoti zilianza kuibuka kuhusu uwezekano wa wawili hao kutengana. Hatimaye, mwezi Machi, Ter Stegen alithibitisha rasmi kuwa ndoa yao ilikuwa imevunjika, ingawa alisisitiza kuwa walitengana kwa amani.

"Baada ya tafakari ya kina, Daniela na mimi tumeamua kuchukua njia tofauti. Kama mnavyoweza kudhani, huu haukuwa uamuzi rahisi, lakini tunaamini ni hatua bora kwetu,"Ter  Stegen alisema wiki jana.

Aliongeza kuwa lengo lao kuu ni kuhakikisha ustawi na mazingira thabiti kwa watoto wao wawili, na kwamba wataendelea kushirikiana kama wazazi huku wakiheshimiana na kuthaminiana kama ilivyokuwa daima.

Kwa sasa, Ter Stegen anaendelea kuwa nguzo muhimu kwa FC Barcelona, huku uvumi kuhusu maisha yake ya kibinafsi ukiwa gumzo kubwa katika vyombo vya habari vya Uhispania.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved