Kombe la Dunia 2030: Mashindano yatafanyika katika nchi sita katika mabara matatu

Uamuzi huo umepangwa kupitishwa kwenye kongamano la Fifa mwaka ujao.

Muhtasari

•Uhispania, Ureno na Morocco zimetajwa kuwa wenyeji, huku mechi tatu za ufunguzi zikifanyika Uruguay, Argentina na Paraguay.

•Saudia Arabia inatarajiwa kuwasilisha ombi la kuandaa michuano hiyo mwaka 2034 kwa mara ya kwanza.

Image: GETTY IMAGES

Kombe la Dunia la 2030 litafanyika katika nchi sita katika mabara matatu, FIFA imethibitisha.

Uhispania, Ureno na Morocco zimetajwa kuwa wenyeji, huku mechi tatu za ufunguzi zikifanyika Uruguay, Argentina na Paraguay.

Mechi za ufunguzi huko Amerika Kusini ni za kuadhimisha miaka 100 kwa Kombe la Dunia kwani itakuwa ni miaka 100 tangu kuanzishwa kwa mashindano hayo huko Montevideo.

Uamuzi huo umepangwa kupitishwa kwenye kongamano la Fifa mwaka ujao.

"Katika ulimwengu uliogawanyika, Fifa na soka vinaungana," alisema rais wa Fifa Gianni Infantino.

“Baraza la Fifa, linalowakilisha ulimwengu mzima wa kandanda, lilikubali kwa kauli moja kusherehekea miaka 100 ya Kombe la Dunia la Fifa, ambalo toleo lake la kwanza lilichezwa Uruguay mnamo 1930, kwa njia inayofaa zaidi.

"Mnamo 2030, tutakuwa na historia ya kipekee duniani, mabara matatu - Afrika, Ulaya na Amerika Kusini - nchi sita - Argentina, Morocco, Paraguay, Ureno, Hispania na Uruguay - kukaribisha na kuunganisha dunia wakati wa kusherehekea pamoja mchezo mzuri, miaka mia moja na Kombe la Dunia la Fifa."

Fifa pia ilithibitisha pia kuwa zabuni kutoka kwa nchi za Shirikisho la Soka la Asia pekee na Shirikisho la Soka la Oceania ndio zitazingatiwa kwa fainali za 2034.

Saudia Arabia inatarajiwa kuwasilisha ombi la kuandaa michuano hiyo mwaka 2034 kwa mara ya kwanza.