Serikali yatoa taarifa chanya kuhusiana na ukarabati wa viwanja vitakavyoandaa AFCON

Hii itakuwa mara ya kwanza mashindano hayo makubwa ya bara kuandaliwa kwenye kanda ya Afrika Mashariki.

Muhtasari

• CAF pia imependekeza kwamba viwanja vinne vya mazoezi virekebishwe ili kutoa vifaa vya kutosha kwa timu na waamuzi

• Tuko katika asilimia 35 ya ukamilishaji kwa sasa, lakini tumehakikishia kwamba viwanja vyote vitakuwa tayari ifikapo Desemba 2025 kama inavyohitajika."Alisema Tum

Uwanja wa Kasarani Picha;Heshima
Uwanja teule wa Kasarani Uwanja wa Kasarani Picha;Heshima
Image: HISANI

Katibu Mkuu wa Michezo Peter Tum ametoa taarifa kuhusu maendeleo ya ukarabati yanayoendelea katika Uwanja wa Kasarani pamoja na uwanja uliopendekezwa wa Talanta.

Kenya, pamoja na majirani wake, Tanzania na Uganda, itakuwa mwenyeji wa Kombe la Mataifa ya Afrika 2027.

Hii itakuwa mara ya kwanza mashindano hayo makubwa ya bara kuandaliwa kwenye kanda ya Afrika Mashariki.

Hivi karibuni, ripoti ya CAF ilibainisha kuwa hakuna uwanja nchini Kenya unaofaa kwa ajili ya majukumu ya kitaifa na kimataifa, hivyo basi kuibua shaka kuhusu nia ya Kenya kutaka kuandaa mojawapo ya mashindano makubwa zaidi duniani.

Hata hivyo, Tum, ambaye kwa sasa anasimamia idara ya michezo kwa muda wakati Rais William Ruto anarekebisha baraza lake la mawaziri, alitoa taarifa kuhusu hali ya viwanja.

Tum amefichua kwamba mbali na viwanja vitatu ambavyo vinakarabatiwa kwa ajili ya matumizi ifikapo wakati wa mashindano, CAF pia imependekeza kwamba viwanja vinne vya mazoezi virekebishwe ili kutoa vifaa vya kutosha kwa timu na waamuzi watakaoshiriki mashindano hayo.

"Tuko vizuri kama nchi. Tulikuwa tunahitaji viwanja vitatu awali, lakini sasa wameamua kwamba tunapaswa kuwa na viwanja vinne vya mazoezi," Tum alisema kwa waandishi wa habari.

"Kama Wizara, tayari tulishatenga Uwanja wa Talanta kama kiwanja kikuu cha AFCON na tukatenga viwanja vinne vya mazoezi hapo.

"Kasarani, pia, tumejipanga kuwa na viwanja vya mazoezi ambavyo tulishaviboresha awali, lakini tunataka kuviboresha zaidi ili viwe tayari kwa mwaka 2027.

Tuko katika asilimia 35 ya ukamilishaji kwa sasa, lakini tumehakikishia kwamba viwanja vyote vitakuwa tayari ifikapo Desemba 2025 kama inavyohitajika."Alisema Tum

Tum pia amefichua mipango kwa ajili ya Uwanja wa Kipchoge Keino Eldoret, ambao utatumika kama ziada kwa viwanja viwili vikuu vya Nairobi.

"Pia kuna kituo Eldoret ambacho tutakitumia kwa AFCON. Tumeainisha viwanja vingine vinne vya mazoezi katika eneo hilo ambavyo tutavifanyia ukarabati."

Tum alifichua kuwa kipaumbele cha serikali ni kuandaa viwanja vikuu kabla ya kuanza ukarabati wa viwanja vya mazoezi, na muda uliowekwa wa mwisho ni Desemba 2025.

"Hatutaki kuharakisha ukarabati wa viwanja vya mazoezi. Kwanza tutakamilisha viwanja vikuu. Kwa ujumla, kama nchi tunadhibiti mambo na hakuna sababu ya wasiwasi."