Beki mpya wa United, Leny Yoro kuwa nje miezi 3 kutokana na jeraha, Hojlund kwa wiki 6

Wote wawili walilazimishwa kutoka katika kipindi cha kwanza cha kichapo cha 2-1 kutoka kwa Arsenal.

Muhtasari

•Leny Yoro atakuwa nje kwa miezi mitatu na mshambuliaji Rasmus Hojlund atakosa wiki sita kutokana na majeraha.

Image: BBC

Beki mpya wa Manchester United aliyenunuliwa kwa pauni milioni 52, Leny Yoro atakuwa nje kwa miezi mitatu na mshambuliaji Rasmus Hojlund atakosa wiki sita kutokana na majeraha waliyoyapata katika mchezo wa kujiandaa kwa amsimu wa Jumamosi dhidi ya Arsenal.

Vyanzo vya habari vilithibitisha habari hiyo zaidi ya saa moja kabla ya United kupata ushindi wa 3-2 dhidi ya Real Betis ya La Liga mjini San Diego.

Wote wawili walilazimishwa kutoka katika kipindi cha kwanza cha kichapo cha 2-1 kwenye Uwanja wa SoFi mjini Los Angeles.

Yoro alirekodiwa katika video akiwa katika kambi ya mazoezi ya United katika Chuo Kikuu cha California, Los Angeles (UCLA), siku ya Jumanne akiwa amevalia kiatu cha kujikinga na kutumia magongo.