
Kocha wa Arsenal, Mikel Arteta, amezungumza na waandishi wa habari kabla ya mechi yao ya Ligi Kuu dhidi ya Leicester City siku ya Jumamosi.
Katika mkutano na wanahabari siku ya Ijumaa, Arteta alithibitisha kuwa winga nyota Bukayo Saka bado yuko katika hatua za awali za kupona jeraha lake, lakini hajapata madhara zaidi katika mchakato wa kupona.
"Saka bado yuko katika hatua za awali za kupona, lakini mpaka sasa hakuna changamoto mpya aliyokumbana nazo," alisema Arteta.
Kauli hii inawapa mashabiki wa Arsenal matumaini kuwa mchezaji huyo muhimu atarejea kikosini hivi karibuni.
Mbali na Saka, Arteta pia alizungumzia hali ya wachezaji wengine walioumia, akiwemo Kai Havertz, ambaye atakosa msimu wote uliosalia kutokana na jeraha la msuli wa paja.
"Tulikuwa na kambi nzuri Dubai – tulikuwa tunajirejesha katika hali, tukifanya mazoezi, na kuungana na mazingira tofauti. Lakini ghafla, jeraha likatokea kwa njia isiyotarajiwa. Ni pigo kubwa kwa sababu ya majeraha tuliyonayo," alisema Arteta, akielezea masikitiko yake kuhusu kuumia kwa Havertz.
Akizungumzia uwezekano wa kusajili mchezaji huru kutokana na changamoto za majeraha, Arteta alisema: “Tunaangazia kila fursa inayopatikana na tutafanya uamuzi kutoka hapo."
Kuhusu sababu za majeraha mengi yanayoikumba timu yake na klabu nyingine msimu huu, Arteta alieleza kuwa ratiba ngumu na mzigo mkubwa wa mechi umekuwa changamoto kubwa kwa wachezaji.
"Kwa mzigo wa mechi na dakika wanazocheza, hili ni jambo lisiloepukika. Ni kama ajali inayosubiri kutokea. Msimu huu, wachezaji wanapitia msongo mkubwa, hasa wale wenye mbinu za kulipuka, na ratiba inafanya iwe vigumu kwao kuhimili," alisema.
Pamoja na majeraha hayo, Arteta anaamini kuwa bado ana wachezaji watakaoweza kuleta ushindani. Alisema atalazimika kubadilisha mbinu za kiufundi ili kukabiliana na hali ya majeraha, lakini anaamini kikosi chake kinaweza kusababisha matatizo kwa wapinzani.
Kuhusu kijana Ethan Nwaneri, Arteta aliashiria kuwa anaweza kucheza kama mshambuliaji wa kati au pembeni kulingana na nguvu zake.
"Ni suala la muda tu – ana sifa zinazofaa kucheza katikati au pembeni. Tunapaswa kuzoea ubora wa wachezaji wetu," alisema.
Kwa upande wa wapinzani wao Leicester City, Arteta aliwasifu na kumtaja kocha wao mpya, Ruud van Nistelrooy, akisema anaijua vyema mbinu zake za kupanga timu.
Katika mjadala wa mbio za ubingwa, Arteta alizungumzia kuhusu Liverpool kupoteza pointi dhidi ya Everton na kusema kuwa hatua hiyo ni chanya kwa Arsenal.
"Unapopunguza pengo, hilo ni jambo chanya. Wiki zijazo zitakuwa muhimu sana katika mbio za ubingwa," alihitimisha Arteta.
Mechi dhidi ya Leicester itakuwa mtihani mkubwa kwa Arsenal, lakini mashabiki wanatumai kurejea kwa wachezaji muhimu kama Saka kutasaidia kuimarisha nafasi yao ya kushindania taji la ligi.