
Nyota wa West Ham United, Michail Antonio, amekutana kwa hisia kali na wahudumu wa dharura waliomokoa maisha yake baada ya ajali mbaya ya gari mwezi Desemba ambayo ilimwacha na mguu uliovunjika na kuleta mashaka kuhusu mustakabali wake wa soka..
Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 35 alikuwa akiendesha gari lake aina ya Ferrari FF alipokosa mwelekeo na kugonga mti katika eneo la Epping Forest. Alikimbizwa hospitalini kwa upasuaji wa dharura na alitumia zaidi ya wiki tatu akiuguza majeraha. Antonio hana kumbukumbu yoyote ya tukio hilo na bado hajarejea uwanjani kuichezea West Ham.
Baada ya miezi kadhaa, Antonio amepata fursa ya kukutana ana kwa ana na watu waliomwokoa — mhudumu wa ambulensi Rob Moon na Dkt. James Moloney.
Katika kipindi cha Morning Live cha BBC siku ya Jumatatu, nyota huyo alitoa shukrani zake kwa dhati wakati wa mkutano wao katika ghala la ambulensi.
"Nataka kusema asante kwa sababu nisingekuwa hapa kama si nyinyi," alisema Antonio. "Kwa hiyo nyinyi ni mashujaa wangu halisi."
Akiwa ameguswa sana, alikiri: "Mimi siwezi kufanya kazi yenu. Nikiona mtu ameumia au ana damu, nitashikwa na hofu au hata kuzimia. Hiyo si kazi niliyoweza kuifanya kamwe."
Ajali hiyo ilitokea katika siku ya dhoruba, ambapo helikopta ya dharura haikuweza kuruka. Moon na Dkt. Moloney walifika kwa gari maalum la dharura na kumkuta Antonio akiwa ndani ya kiti cha nyuma cha gari, akionekana kujaribu kutoka. Walimtambua haraka na kushughulikia jeraha lake la mguu lililovunjika.
Hata katikati ya hali hiyo ya dharura, waliweza kumtuliza kwa kumzungumzia masuala ya soka, maisha yake ya kitaaluma na kumbukumbu zake muhimu uwanjani. “Tunawatibu wote kwa usawa,” alisema Dkt. Moloney, “lakini si watu wengi wana jezi yenye jina lao mgongoni.”
Antonio alikiri kuwa athari za kiakili bado ni kubwa. “Kimwili ninasonga mbele, lakini kiakili, mshtuko wa ajali unachukua muda mrefu kuponyeka. Familia yangu waliumia zaidi – wao waliniona nikiwa hospitalini, nikiwa sijitambui. Sina kumbukumbu, lakini wao wanazo. Wao waliishi tukio hilo.”
Hata hivyo, Antonio bado ana matumaini ya kurejea uwanjani na
anaamini kuwa anaendelea vyema kuliko ilivyotarajiwa katika safari yake ya
kupona.