logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Onana aingia kwenye vita kali vya maneno na Matic huku akitajwa miongoni mwa kipa duni zaidi Man United

Mzozo huo ulianza baada ya Onana kueleza kuwa Man United ni “bora zaidi” kuliko Lyon.

image
na Samuel Mainajournalist

Football10 April 2025 - 09:10

Muhtasari


  • Kauli hiyo ilimkera Matic ambaye sasa ni kiungo wa Lyon, na hakusita kumshambulia vikali Onana wakati wa mkutano na wanahabari.
  • Onana  alijibu kwa maneno yaliyodai kuwa hakudhamiria kuidharau Lyon, huku akijivunia mafanikio yake binafsi akiwa na United.

Nemanja Matic wanakabiliana na Andre Onana

Kipa wa Manchester United, Andre Onana, amejipata katika vita vya maneno na kiungo wa zamani wa klabu hiyo, Nemanja Matic, baada ya kutofautiana kuhusu ubora wa kikosi cha United kulinganisha na Lyon ya Ufaransa.

Mzozo huo ulianza baada ya Onana kueleza kuwa Man United ni “bora zaidi” kuliko Lyon, kabla ya timu hizo kukutana kwenye robo fainali ya Ligi ya Europa.

Kauli hiyo ilimkera Matic ambaye sasa ni kiungo wa Lyon, na hakusita kumshambulia vikali Onana wakati wa mkutano na wanahabari siku ya Jumatano.

“Namheshimu kila mtu, lakini ili kusema maneno kama hayo, unahitaji kuwa na msingi wa kuyasema,” alisema Matic.
Aliongeza “Kama wewe ni mmoja wa makipa duni zaidi katika historia ya Manchester United, unapaswa kuwa makini na kauli zako. Kama ingekuwa Van der Sar, Schmeichel au De Gea wameyasema hayo, ningefikiria mara mbili. Lakini kwa mtu kama huyo, haikubaliki.”

Onana hakukaa kimya. Kupitia mtandao wa X (zamani Twitter), alijibu kwa maneno yaliyodai kuwa hakudhamiria kuidharau Lyon, huku akijivunia mafanikio yake binafsi akiwa na United.

“Kamwe singewahi kuidharau klabu nyingine,” aliandika Onana.
“Tunajua mechi ya kesho itakuwa ngumu dhidi ya wapinzani imara. Lengo letu ni kuandaa mchezo bora kwa ajili ya kuwapa mashabiki wetu furaha. Angalau mimi nimebeba mataji na klabu bora zaidi duniani — si kila mtu anaweza kujivunia hilo,” aliongeza

Onana alijiunga na Manchester United mwaka 2023 akitokea Inter Milan kwa dau la pauni milioni 47.2. Hadi sasa, amecheza mechi 93 na kuweka clean sheets 23, na pia ameshinda Kombe la FA.

Hata hivyo, msimu wake wa kwanza Old Trafford umekumbwa na lawama nyingi kutokana na makosa ya mara kwa mara golini, hali iliyomfanya akosolewe vikali na baadhi ya mashabiki.

Kwa upande wake, Nemanja Matic alichezea Manchester United kati ya mwaka 2017 hadi 2022 na kuonekana mara 128. Alikuwa na mafanikio makubwa akiwa Chelsea ambako alishinda mataji mawili ya Ligi Kuu ya England, Kombe la FA na EFL Cup. Baada ya hapo, aliitumikia AS Roma na Rennes kabla ya kujiunga na Lyon mwaka huu.

Kwa sasa, Manchester United wapo katika nafasi ya 13 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya England, na Ligi ya Europa ndiyo nafasi yao ya mwisho kujiokoa msimu huu chini ya kocha Ruben Amorim.


Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved