Patanisho: 'Bwanangu aliniacha nyumbani akarudi Nairobi kuchumbia msichana wa Facebook' Mwanadada asimulia masaibu ya ndoa yake

Muhtasari

•Mama Precious alieleza kwamba alifumania mumewe akiwa na mpango wa kando mwaka uliopita na kudai kuwa inagwa bado hawajatengana, roho yake haijawahi pata utulivu tangu wakati ule.

•Alieleza kuwa mumewe alikuwa anasita kushika zake kila alipompigia usiku na hapo ndipo akaanza kushuku kuwa kuna kitu kibaya ambacho kilikuwa kinaendelea

•Vincent alijitetea kwamba mwanadada ambaye mkewe alishuku kuwa mpango wake wa kando alikuwa dobi ambaye alikuwa ameenda kumfulia nguo kwa siku moja tu.

Gidi na Ghost
Gidi na Ghost
Image: RADIO JAMBO

Katika kipindi chetu cha Gidi na Ghost asubuhi kitengo cha 'Patanisho', mwanadada aliyejitambulisha kama Mama Precious (24) kutoka Kibra alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mume wake Vincent Kigunzu (32).

Mama Precious alieleza kwamba alifumania mumewe akiwa na mpango wa kando mwaka uliopita na kudai kuwa inagwa bado hawajatengana, roho yake haijawahi pata utulivu tangu wakati ule.

Alisema kuwa wamekuwa kwa ndoa kwa kipindi cha miaka minne na tayari wamebarikiwa na watoto wawili.

"Tumekuwa kwa ndoa miaka minne. Mwezi wa tisa mwaka uliopita mume wangu aliniambia kuwa hatungewezana na maisha ya Nairobi kwa sababu ya Corona turudi nyumbani. Mimi nikakubali tuende nyumbani. Tukaenda nyumbani tukakaa huko. Kufika mwezi wa kumi na moja, akaniambia eti ameona kama kwamba amelemewa na maisha ya nyumbani, akadai arudi Nairobi aende atafute.

Mimi nilisema enyewe mwanaume ni wangu na tumetoka mbali na yeye. Nikamwambia arudi Nairobi, kumbe alikuwa amepata msichana wa Facebook. Yeye kurudi Nairobi akaanza kuchumbiana na huyo msichana" Mama Precious alisimulia.

Alieleza kuwa mumewe alikuwa anasita kushika zake kila alipompigia usiku na hapo ndipo akaanza kushuku kuwa kuna kitu kibaya ambacho kilikuwa kinaendelea.

Mama Precious alisema kuwa aliamua kufunga safari ya kuelekea Nairobi kubaini kilichokuwa kimetia doa kwa ndoa yao mwezi Aprili mwaka huu.

"Niliona hata simu zangu hataki kushika. Vile ilifika mwezi wa nne  nikatafuta nauli nikakuja Nairobi. Kufika Nairobi, kumbe alikuwa ameleta huyo msichana kwa nyumba mwezi wa tatu wakakaa hadi mwezi wa nne. Huyo msichana alikuwa ameenda shughuli zingine nilipofika.. Ilibidi nitoke kwanza niende" Alisimulia Mama Precious.

Mama Preciouss alieleza kwamba alirudi kwa mumewe mwezi mmoja uliopita ila bado roho yake haijatulia kutokana na yaliyokuwa yametendeka hapo awali. Alihofia kuwa mumewe bado anaendelea na tabia za kuhusiana na mipango ya kando.

Vincent alipopigiwa simu alisema kuwa matendo yake ya hapo awali yalikuwa yamechangiwa na hasira kubwa kwa mke wake. Alimsihi mkewe asahau yaliyokuwa yamepita.

"Yale ambayo yalipita nilikwambia tuachane nayo maanake wakati wa COVID tulienda wote nyumbani wakati kibarua iliissha. Lakini wakati nilirudi yake yote ulikuwa umenifanyia ndio yakafanya nichukue hatua nyingine" Vincent aliarifu mkewe.

Mama Precious alisema kuwa alichoma nguo za mumewe kutokana na hasira baada ya kugundua kuwa alikuwa na mpango wa kando.

Vincent alijitetea kwamba mwanadada ambaye mkewe alishuku kuwa mpango wake wa kando alikuwa dobi ambaye alikuwa ameenda kumfulia nguo kwa siku moja tu.

"Wakati ulienda ulikuwa umeniambia eti nioe msichana mwingine na ukaniambia eti hutawahi rudi ata siku moja na ukafuatanisha na matusi. Mimi nikaona ni sawa lakini sikukutusi. Msichana ambaye alikuja alikuwa wa kufua nguo. Alikuja kufua nguo siku moja tu. Huwa halali kwa nyumba" Vincent alidai.

Vincent alidai kwamba anampenda mkewe sana na kueleza kuwa alimkubali tena wakati alirejea nyumbani Aliahidi kuwa hatajihusisha tena na mipango wa kando na hata akakubali kula kiapo hewani.