Patanisho: “Nilimpiga mama mkwe alipoingilia kati ugomvi na mume wangu, naomba anisamehe!”

“Tulikosana na bwanangu akanichapa ndio mama mkwe akaingilia akaona nitapiga mtoto wake nimuumize akachukua mwiko akanichapa nikaona wataniumiza nikamchapa pia" alisema.

Muhtasari

• Wakati huo, Sylvia alikuwa na mimba ya miezi 7 na mashemeji zake walipokuja jioni kutaka kumchapa, ndugu zake walikuja na kumchukua na kurudi nyumbani.

• Alisema angependa kumuomba msamaha mama mkwe ili kurudisha mtoto kwao, akisema kwamba mtoto Analia sana na kila mtu anamwambia kwamba kosa ni kumchapa mama mkwe.

GIDI NA GHOST.
GIDI NA GHOST.
Image: RADIO JAMBO

Katika kitengo cha Patanisho kwenye Radio Jambo, mrembo kwa jina Sylvia mwenye umri wa miaka 23 alitaka kupatanishwa na mama mkwe Ruth mwenye umri wa miaka 58.

Sylvia alieleza kwamba walikosana Julai 2022 baada ya mama mkwe kuingilia kati ugomvi wake na mumewe.

Mrembo huyo alisema kwamba walikosana na mumewe kwa ndoa na wakati wa ugomvi wao ambao uligeuka na kuwa vita, mama mkwe aliingilia kati kusaidia mwanamwe baada ya kuona Sylvia alikuwa amemlemea kwa vita.

Hapo ndipo mama mkwe alimchapa Sylvia kwa kofi na Sylvia kwa hasira akaamua kujibu mipigo kwa kumshambulia mama mkwe kwa kichapo kikali hadi kumkimbiza hadi kwa nyumba yake na kumzidishia kichapo zaidi.

Wakati huo, Sylvia alikuwa na mimba ya miezi 7 na mashemeji zake walipokuja jioni kutaka kumchapa, ndugu zake walikuja na kumchukua na kurudi nyumbani.

Alisema angependa kumuomba msamaha mama mkwe ili kurudisha mtoto kwao, akisema kwamba mtoto Analia sana na kila mtu anamwambia kwamba kosa ni kumchapa mama mkwe.

“Tulikosana na bwanangu akanichapa ndio mama mkwe akaingilia akaona nitapiga mtoto wake nimuumize akachukua mwiko akanichapa nikaona wataniumiza nikamchapa pia nikamfuata hadi kwake tukapigania kwake tukajifungia kwa nyumba,” alisema.

“Hapo ndio tukakosana kesho yake wakaita ndugu zangu wakakuja tukaonge tukamaliza jioni wakaita mashemeji jioni kuja kunichapa ndugu zangu wakanikujia usiku nikaenda nyumbani nikajifungua nikaleta mtoto anyolewe, sasa hivi mtoto ni mgonjwa Analia sana, nataka kuomba mama mkwe msamaha juu kila mtu ananiambia nilichapa mama mkwe nilikosea,” aliongeza.

Kwa upande wake Ruth, alisema, “Mama msamaha inaombewa kwa kanisa mbele ya madhabahu kama tuko wote wazazi na bwanako mbele ya Mungu. Sijakataa nimekubali lakini wacha tuone.”

Mama mkwe hata hivyo alifichua kwamba Sylvia alirudiana na mumewe na kumfuata anakofanya kazi na kutaka kumshambulia kwa kisu, jambo ambalo mama mkwe anasema ni la kukera.

“Msichana mwenyewe tulikuwa tumemkubali vizuri lakini tabia tu ndio ilitushinda, hata hapa kwangu alikuwa hajakaa mwaka mmoja, wakigombana na bwanake anachukua kisu tu anataka kumdunga, tukaona hawa wakikaa wakipata watoto watauana,” alisema.

Alisema kwamba hana haja ya Sylvia bali angependa aendelee kulea mwanawe hadi pale atakuwa umri sahihi wa kurejeshwa kwa baba yake.