In Summary

• Makena Ngugi alisema kwamba hii ndio mara yake ya kwanza kupiga kura na alifurahishwa na mchakato huo licha ya kukumbwa na changamoto kiasi.

Bintiye mwakilishi wa kike Nairobi, Esther Passaris, Makena Ngugi amewafurahisha wanamitandao kwa lafudhi yake ya Kiingereza cha Marekani isiyo na doa.

Makena Ngugi alikuwa anazungumza na wanahabari pindi tu baada ya kupiga kura katika kituo cha shule ya msingi ya Farasi Lane na kufurahia kwamba hatimaye amepiga kura yake kwa mara ya kwanza.

Alidokeza kwamba licha ya kuwa na furaha ya kushiriki haki yake ya kidemokrasia kwa mara ya kwanza ila upigaji kura huo ulikuwa kwa mwendo wa kobe sana.

“Mchakato wa kupiga kura ulikuwa kidogo hauna kasi na na pia kulikuwa na baadhi ya makosa lakini tunaomba yatarekebishwa kwa muda sahihi ili kila Mkenya aweze kupiga kura yake na mchakato huu kukamilika vizuri,” bintiye Esther Passaris alisema kwa mbwembwe.

Msichana huyo mwenye urembo wa aina yake pia alionekana kumpigia debe mgombea mwenza wa Azimio la Umoja pale ambapo aliwarai wanadada wote kwa kuwaambia kwamba uchaguzi huu una umuhimu mkubwa kwa watoto wa kike na kusema kwamab litakuwa jambo zuri kama watajaribu safari hii na kumchagua naibu rais mwanamke, ambaye ni Martha Karua.

“Tunaweza kuwapigia kura wanawake ikizingatiwa kuwa ni wanawake ambao wamekuwa wakifanya kazi kwa bidii na hii ndiyo fursa ambayo Kenya inapata kumchagua naibu rais mwanamke,” aliongeza

Passaris anawania kutetea nafasi yake kama mwakilishi wa wanawake Nairobi kupitia tikiti ya chama cha ODM huku tafiti za awali zikimuweka kifua mbele ya mshindani wake mkuu kutoka UDA, Millicent Omanga.

View Comments