
Radio Jambo, kituo chetu pendwa kinachoongoza kwa usikilizaji kote nchini, kimepokea uteuzi wa kipekee katika Thamani Awards 2025, kikiorodheshwa kwenye kipengele cha Best Mothers’ Station.
Hii ni tuzo inayotambua mchango mkubwa wa vyombo vya habari katika kuinua sauti, ustawi na mafanikio ya akina mama nchini Kenya.
Katika mafanikio haya, malkia wetu wa Swahili Radio—Massawe Japanni—ambaye huendesha kipindi maarufu cha Bustani la Massawe, pia ameteuliwa kwenye kipengele cha Best Media Personality.
Massawe ambaye ana sauti na ushawishi wa kipekee ameungana na majina makubwa katika tasnia ya habari kama Lulu Hassan, Victoria Rubadiri na Yvonne Okwara, katika kushindania heshima hiyo.
Kwa mujibu wa mkurugenzi wa tuzo hizo, Esther Wairimu Kiai, Thamani Awards zinalenga kusherehekea nguvu na mchango wa kina mama si tu ndani ya familia, bali pia katika nyanja za jamii, siasa, biashara na teknolojia.
“Tunaenzi majukwaa ambayo yamekuwa nguzo ya kina mama. Radio Jambo ni mfano wa chombo kinachoshiriki kikamilifu katika ujenzi wa familia kupitia maudhui yenye kugusa maisha ya watu,” alisema Kiai.
Katika orodha ya mwaka huu, baadhi ya vipengele vilivyovutia hisia kubwa ni:
- Chapa Bora ya Urembo (Best Beauty
Brand): ambapo majina kama Huddah Monroe, Joanna Kinuthia (Joanna K
Cosmetics) na Phiona Wambui yamejumuishwa.
- Mchezaji Bora wa Mwaka (Sports
Personality): Mashujaa wa michezo kama Faith Kipyegon, Mwanalima Adam, na
Beatrice Chebet wamepata nafasi ya kushindania heshima hiyo.
- Mshawishi bora wa Mitandaoni (Best
Social Media Impact): Majina kama Elsa Majimbo, Shakira Wafula na Samira
Sanuura yanang’ara kwa ushawishi wao wa kidijitali.
- Mburudishaji Bora wa Mwaka (Entertainer
of the Year): Majina kama Awinja, Femi One na Nadia Mukami yanaongoza
orodha ya burudani.
- Mshawishi Bora Kenya 2025 (Best
Influencer KE 2025): Wasanii na wanamitandao maarufu kama Akothee, Azziad
Nasenya, na Betty Kyallo wanachuana vikali.
- Sauti ya Hekima 2025 (Voice of Reason 2025): Kipengele kinachoweka mbele wanawake viongozi mashuhuri wakiwemo Millie Odhiambo, Gathoni wa Muchomba, na Zamzam Mohamed kwa mchango wao katika uongozi na mabadiliko ya kijamii.
Kipindi cha upigaji kura kitaendelea
hadi Mei 5, na washindi watatangazwa rasmi katika hafla ya kifahari
itakayofanyika Mei 11, 2025—Siku ya Akina Mama—katika KCB Leadership
Centre, Karen, Nairobi.
Mashabiki wameombwa kuonyesha mshikamano na chapa zao pendwa kwa kupiga kura na kusherehekea sauti zinazogusa maisha ya familia zetu kila siku.
Tembelea www.thamaniawards.com
kupiga kura au kupata maelezo zaidi.