Bunge la Kaunti ya Nairobi hatimaye limeidhinisha uteuzi wa Anne Kananu Mwenda kuwa Naibu Gavana.
Kwenye kikao cha bunge hilo Ijumaa, madiwani waliohudhuria waliidhinishwa ripoti ya Kamati ya Uteuzi ambayo awali, asubuhi, ilimchunguza Bi Mwenda kubaini ufaafu wake kwa wadhifa huo.
Kabla ya uteuzi wake mapema 2020 na gavana wa zamani Mike Sonko, Bi Mwenda amekuwa Afisa Mkuu katika Idara ya Kupambana na Majanga katika serikali ya kaunti ya Nairobi.
Kwa mujibu wa ripoti ya kamati hiyo iliyowasilishwa bunge na kiongozi wa wengi Abdi Guyo, Bi Mwenda aliidhinishwa na asasi hitajika za serikali kama vile Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru Nchini (KRA), Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC), Bodi ya Kutoa Mikopo kwa Elimu ya Juu (HELB) na Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI).
Kamati hiyo ilibaini kwamba Kananu ametimiza matakwa mengine yote hitajika kwa wadhifa wa Naibu Gavana wa Kaunti ya Nairobi.
Baada ya Kananu kuapshwa aliahidi kuunga ripoti ya mpango wa maridhiano BBI mkono huku akisema kwamba atafanya kazi na NMS ili kuhakikisha mataka ya wakazi wa Nairobi yametimizwa.
Vile vile, alidai kuwa shida nyingine ambayo ilikuwa ikiwaathiri mawaziri na maafisa wakuu wa serikali ya kaunti ya Nairobi ni vitisho vya kila mara kutoka kwa Gavana wa zamani Mike Sonko.