

INSPEKTA Jeneraliw a polisi Douglas Kanja amevunja kimya chake baada ya vituo bandia vya polisi kugunduliwa katika kaunti za Uasin Gishu na Kakamega katika siku chache zilizopita.
Akizungumza na waandishi wa Habari Jumatano,
Kanja alisisitiza kwamba ni makosa makubwa kwa raia kuchukua hatua ya kufungua
kituo cha polisi bila kufuata taratibu husika.
“Mtu ambaye alifungua stesheni yake,
kituo cha polisi, kwanza mimi niseme hayo ni makosa makubwa maana kuna taratibu
zile zinafuatwa, wananchi wa hapa kwa mfano wakitaka kituo cha polisi, kuna
utaratibu ambao utafuatwa,” Kanja alisema.
Mkuu huyo wa idara ya polisi alieleza
kinagaubaga taratibu ambazo zinafaa kufuatwa ili kuanzisha kituo cha polisi
katika eneo lolote ndani ya mipaka ya Kenya.
“Kuna kitu ambacho kinaitwa public
participation, Pamoja na uongozi wa eneo Fulani ambayo wenyewe wanaona ni kweli
tunahitaji kituo cha polisi ndio tuweze kuongeza usalama, halafu hilo pendekezo
linapelekwa kwa kamati ya usalama kwenye sub-county, ambayo inaongozwa na DCC
na wakuu wa polisi wa hilo eneo, na wale wengine ambao wako katika vitengo
mbalimbali vya usalama.”
“Wanaikalia chini hiyo ripoti vile
wananchi wanapendekeza kama kweli kituo cha polisi kinahitajika eneo hilo. Hilo
wazo linaletwa mpaka linafika kwa inspekta jenerali wa polisi kule Nairobi na
kweli sisi tukifuata ule utaratibu umewekwa na Katiba yetu, tunaona kweli
inatakikana kuletwa kituo cha polisi hapa. Huo ndio utaratibu unaostahili kufuatwa
na yule aliyefungua kituo chake cha polisi angefuata hivyo,”
Kanja alitoa maelezo ya kina.
Taarifa hii inajiri siku chache tu baada
ya mwanamume wa umri wa miaka 26 kufungua kituo binafsi cha polisi kijijini
Cheboror kaunti ya Uasin Gishu.
Habari zinasema kuwa mtuhumiwa Collins
Leitich, almaarufu Chepkulei, mkazi wa Kijiji cha Asis eneo la Ndugulu,
alijitwika jukumu la kuanzisha kituo cha polisi cha doria kwenye jengo moja, na
kufikia kupaka rangi jengo hilo kwa rangi rasmi za polisi, na hivyo kujenga
hisia ya kituo halali cha ulinzi.
Kama hilo halitoshi, Jumatano kuliibuka
ripoti zingine za kundi la vijana ambao walikuwa wanaendesha seli bandia ya
polisi katika kaunti ya Kakamega.
Kundi hilo lilikuwa linawakamata na
kuwazuilia wananchi katika vyumba vilivyotelekezwa na kuwatoza faini ya
shilingi 300 ili kuwaachilia huru.