logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Pigo kwa Super Metro NTSA ikipiga marufuku magari ya sacco hiyo kutoka barabarani

NTSA ilionya watu dhidi ya kuabiri gari lolote la sacco hiyo huku agizo likitolewa kwa maafisa wa Trafiki kuyazuia magari yao yote yatakayopatikana yakibeba abiria barabarani.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Habari20 March 2025 - 11:07

Muhtasari


  • NTSA ilitaarifa umma kwamba sacco hiyo yenye magari ya uchukuzi wa umma zaidi ya 500 yamepigwa marufuku kutoka barabarani 
  • NTSA ilionya watumizi wa usafiri wa umma dhidi ya kuabiri gari lolote la sacco hiyo huku agizo likitolewa kwa maafisa wa Trafiki kuyazuia magari yao yote 

Super Metro

MAMLAKA ya kitaifa ya usafiri na usalama barabarani NTSA imetangaza kupiga marufuku kampuni ya magari ya Super Metro ambayo hufanya biashara ya uchukuzi wa umma jijini Nairobi na kaunti majirani.


Kupitia tangazo lililochapishwa kupitia ukurasa wao wa X, NTSA ilitaarifa umma kwamba sacco hiyo yenye magari ya uchukuzi wa umma zaidi ya 500 yamepigwa marufuku kutoka barabarani hadi pale watakapozingatia kikamilifu Kanuni za Magari ya Utumishi wa Umma ya 2014 na masharti mengine yaliyowekwa.


“Hii ni kuufahamisha Umma kwamba Mamlaka imesimamisha leseni ya waendeshaji wa Super Metro Limited hadi Kampuni itii kikamilifu Kanuni za Magari ya Utumishi wa Umma, 2014 na masharti mengine yaliyowekwa,” sehemu ya chapisho hilo ilisema.


NTSA ilionya watumizi wa usafiri wa umma dhidi ya kuabiri gari lolote la sacco hiyo huku agizo likitolewa kwa maafisa wa Trafiki kuyazuia magari yao yote yatakayopatikana yakibeba abiria barabarani.


“Wananchi wametahadharishwa dhidi ya kupanda gari la kampuni ya Super Metro Limited. Idara ya Trafiki inahitajika kukamata magari ya Kampuni ambayo yatapatikana yakifanya kazi kinyume na kusimamishwa,” tangazo hilo lilisomeka zaidi.


Haya yanajiri siku chache kufuatia tukio la kuhuzinisha ambapo mwanamume wa umri wa makamo aliripotiwa kufa baada ya kudaiwa kusukumwa kutoka ndani ya moja ya gari la sacco ya Super Metro likiwa katika mwendo wa kasi.

Kulingana na NTSA ilifanya uchunguzi wa kina kwenye Super Metro na kubaini kuwa kati ya magari yake 523, 15 yalikuwa na vyeti vya ukaguzi vilivyokwisha muda wake na 8 kati yao yalikuwa na Leseni za Huduma za Barabarani (RSL) zilizoisha muda wa matumizi.

NTSA pia iligundua kuwa madereva kadhaa kutoka SACCO hawafikii vigezo vinavyohitajika jambo ambalo linaleta hatari kubwa ya usalama.

Kabla ya leseni ya uendeshaji kurejeshwa Super Metro imeombwa kuwasilisha magari 294 yenye ukiukaji kwa ukaguzi wa utiifu katika kituo cha Ukaguzi wa Magari cha Likoni na kupata ripoti za kufuata sheria za magari yote.

Ni lazima pia iwasilishe madereva 42 kati ya 109 walio na ukiukaji wa kasi ili wajaribiwe tena katika Kituo cha Majaribio ya Madereva Likoni.

Hii ni baada ya madereva 64 kutoka Super Metro kushindwa kufanya majaribio tena mnamo Machi 10, na kusababisha kusitishwa kwa leseni zao za udereva.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved