

WAZIRI wa zamani wa elimu ya masuala ya usalama wa ndani, Dkt Fred Matiang’i ametua nchini usiku wa Alhamisi.
Matiang’i ambaye amekuwa akisemekana kulenga
urais wa 2027 kwa tikiti ya chama cha Jubilee alilakiwa na viongozi mbalimbali
wa kisiasa kutoka eneo la Gusii lakini pia katibu mkuu wa chama hicho.
Katika picha ambazo zimechapishwa mitandaoni,
Matiang’i alionekana mwingi wa furaha Pamoja na katibu wa Jubilee Jeremiah
Kioni, seneta wa Kisii Richard Onyonka miongoni mwa wengine ambao wamekuwa
wakimpigia debe.
Kwa muda mrefu sasa, Matiang’i ambaye ni
mwandani wa rais mstaafu Uhuru Kenyatta amekuwa akisemekana kulenga kutwaa
uongozi wa ikulu katika uchaguzi wa 2027 japo mwenyewe hajawahi sikika akitamka
kuhusu azma hiyo.
Ujio wake unatarajiwa kubadilisha kabisa
mawimbi ya siasa za humu nchini kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027, ambapo Matiang’i
huenda akaungana na wanasiasa wengine wengi kwa lengo la kumng’atua rais Ruto
mamlakani kupitia kura za urais 2027.
"Mifumo yote iko tayari sasa!,"
Jubilee ilichapisha kwenye kurasa zake rasmi.
Kioni, haswa, amesisitiza mara kwa mara
Matiangi kuongoza chama katika kinyang'anyiro kifuatacho cha uchaguzi.
Pia alionya dhidi ya majaribio ya kukwamisha
azma ya Matiangi ya kisiasa, akisisitiza kuwa juhudi zozote za kumzuia hatimaye
zitafeli.
Hata hivyo, wapinzani wa rais Ruto hawatakuwa
na kibarua rahisi kumng’atua mamlakani wasipojipanga kwa njia sahihi.
Tayari rais Ruto ameweka wazi kwamba yuko
tayari kumenyana na yeyote atayaeleng’a kumng’atua ofisini kupitia kwa kura,
akionyesha matumaini kwamba wananchi watampa muhula wa pili kwa kuzingatia miradi
ya maendeleo ambayo anapanga katika sehemu mbalimbali nchini.
Matiang’i sasa anatarajiwa kuungana na
wapinzani wengine wa serikali akiwemo Kalonzo, Gachagua, Wamalwa, Karua, Omtatah na
Kebaso kwa lengo la kutwaa ushindi 2027.