
Rais William Ruto amemsifu Naibu wake Kithure Kindiki, akisema anatekeleza majukumu yake vizuri, tofauti na Naibu Rais wa zamani Rigathi Gachagua ambaye, kwa mujibu wa Rais, huzungumza sana bila kufanya kazi ya maana.
“Mara ya kwanza nimepata naibu ambaye anaelewa kazi na ananisaidia kuisukuma, si mtu wa pang’ang’a,” alisema Ruto.
Rais Ruto alisema hatatishwa na watu wanaomwambia kuwa atahudumu kwa muhula mmoja tu.
“Nimekuwa kwenye siasa kwa miaka mingi. Siwezi kutishwa na mtu yeyote. Kutishwa? Watisheni wengine,” alisema Ruto.
Alisema serikali yake imepiga hatua kubwa tangu iingie madarakani mwaka 2022.
“Mlinipa nafasi ya kuongoza Kenya na mkanieleza mngependa nirekebishe uchumi, kilimo, elimu, ajira na afya. Nimeona ripoti ya kazi mliyonipa na ninafuraha kuripoti kwamba tumewaajiri walimu 76,000 na kabla ya Januari, tutaajiri wengine 24,000,” alisema.
Aidha, alisema kuwa serikali imepiga hatua kubwa katika kubadilisha vyuo vikuu vya humu nchini.
“Matatizo ambayo vyuo vikuu vilikuwa navyo yamepatiwa suluhisho kwa kuweka mfumo mpya wa ufadhili unaomlenga mwanafunzi, na sasa vyuo vikuu vinaweza kufundisha watoto wetu na kuwalipa wahadhiri,” alisema.
Kuhusu sekta ya kahawa, Rais Ruto aligusia suala la magenge ya kihalifu, akisema:
“Tulikuwa na watu waliokuwa wakitumia nguvu kuhusu kahawa,” akionyesha nia ya kushughulikia matatizo ya wakulima katika sekta hiyo.