
Seneta wa Nyandarua, John Methu, amesema hataki Rais William Ruto kuhudhuria mazishi yake endapo atafariki dunia.
Akizungumza Jumanne, Julai 1, 2025, wakati wa ibada ya mazishi ya Mheshimiwa Beth Waitho Njoroge, Mwakilishi Mteule wa Bunge la Kaunti ya Nyandarua, Methu alitangaza kwamba hata akifungwa, msimamo wa wananchi hautatetereka na kwamba athari za muhula wa pili kwa rais zitakuwa mbaya kwa taifa.
“Ikinitokea nife, ni lazima mnizike kwa heshima, na yeye asihudhurie mazishi yangu.”
Seneta huyo aliendelea kwa kumtuhumu rais kwa kuwalenga makusudi wanasiasa wanaompinga kisiasa, akiwemo Naibu Rais wa zamani Rigathi Gachagua pamoja naye binafsi, kupitia vitisho na hofu.
Hata hivyo, alisisitiza kuwa mbinu kama hizo hazitavunja ari ya wafuasi wao.
“Haijalishi unamfanyia nini Rigathi Gachagua, wewe Ruto. Haijalishi unafanya nini kwa mimi John Methu. Sijali. Lakini ukinifunga leo, hawa watu walioketi hapa bado watakurejesha nyumbani.”
Seneta Methu alimwambia Rais kwamba hata akitumia nguvu dhidi yake, kama vile kumpiga risasi kichwani, bado wananchi hawataacha kumwajibisha.
Alisema Rais Ruto anapaswa kuelewa kuwa watu wameazimia kwa dhati kumrejesha nyumbani, akisisitiza kuwa hatima yake ya kisiasa tayari imeamuliwa bila kujali mbinu atakazotumia.
“Ukipitisha risasi kwenye kichwa changu, haijalishi. Hawa watu bado watakurejesha nyumbani.”
Seneta huyo alieleza kuwa majibu ya Rais kwa wakosoaji wake yanawapa moyo zaidi badala ya kuwavunja.
“Kadri anavyojibu, ndivyo anavyotutia ujasiri zaidi. Kama mimi sasa, kichwa changu hakiwezi kupasuliwa,” alieleza.
Seneta Methu pia alisimulia tukio binafsi ambapo nusura akamatwe na maafisa wa usalama, akisema alikaribia kushikwa lakini alifanikiwa kukwepa kwa kubadilisha magari haraka.
Alitafakari tukio hilo akisema lilionyesha jinsi alivyo imara, na kuongeza kuwa hata wale waliokusudia kumkamata walishangazwa alipowaanza kuimba kwa ujasiri maneno ya “wantam” kabla ya kutoroka.
“Niliwahi kukaribia kushikwa na maafisa, lakini nikaruka kwenye gari moja, kisha nikaingia jingine na nikasema, ‘One term.’”