
Nairobi, Kenya, Julai 23, 2025 — Kiongozi wa chama cha People’s Liberation Party (PLP), Martha Karua, akiwa jijini Nairobi, amemkosoa vikali kiongozi wa ODM Raila Odinga kwa kupendekeza kuanzishwa kwa kikao kikuu cha kitaifa (‘national conclave’), akisema ni hila ya serikali ya Rais William Ruto ya “kuwadanganya wananchi.
“Majadiliano na utawala dhalimu wa Kenya Kwanza siyo chaguo. Nilitaka kumkumbusha rafiki yangu Raila kwamba aliunga mkono mazungumzo ya NADCO ambayo mimi nilipinga,” alisema Karua katika mahojiano na runinga ya NTV Jumatano usiku.
“NADCO haikuwasaidia wananchi”
Karua alisema kuwa pendekezo la ‘conclave’ ni mwendelezo wa mikakati ya kisiasa isiyokuwa na manufaa kwa mwananchi wa kawaida, akitolea mfano jopo la NADCO la 2023.
“Walikuwa wamesema litachukua siku 90 lakini likadumu kwa mwaka mzima. Matokeo yake hayakuwa kwa manufaa ya wananchi. Isipokuwa viti kwa wakubwa, hakuna kilichowanufaisha wananchi. Gharama ya maisha bado iko juu,” alisema Karua.
Alisisitiza kuwa Rais Ruto hana nia ya kweli ya kushughulikia matatizo ya wananchi.
“Tunachohitaji leo ni utawala wa sheria. Si hadithi, si uongo. Ni utii kwa sheria,” aliongeza.
Karua amkosoa Ruto kuhusu kifo cha Ojwang’
Karua alizungumzia kifo cha mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang’ aliyefariki akiwa mikononi mwa polisi baada ya kugongana na Naibu Mkuu wa Polisi, Eliud Lagat. Alilaani kimya cha serikali kuhusu suala hilo.
“Hatujaambiwa matokeo ya uchunguzi. Lakini Ojwang’ alikufa kwa sababu ya malalamiko ya Lagat. Anawezaje kurudishwa kazini bila haki kufanyika? Hii ni dhuluma na dharau ya wazi ya serikali ya Kenya Kwanza,” alisema akiwa katika ofisi za chama cha PLP, Nairobi.
Atoa wito kwa Raila kujiondoa
Karua alisimulia jinsi alivyoongea kwa simu na Raila baada ya maandamano ya Saba Saba mnamo Julai 7, akimtaka ajiondoe kwenye ushirikiano wowote na utawala wa Ruto.
“Nilimwambia, kama mtu ambaye amepigania haki za wananchi kwa miaka mingi, anawezaje kuvumilia umwagikaji damu unaoendelea? Nilimwomba ajitoe, aache kuunga mkono utawala huu wa dhuluma.”
Alidai Raila hakukubali kukutana naye ana kwa ana na badala yake alieleza kuwa ‘conclave’ imeeleweka vibaya.
“Nilimwambia naenda Marekani. Sina haja ya mkutano wowote kuhusu haya mambo. Ruto anatumia haya mazungumzo kuwafanya wananchi waamini kuna mabadiliko, ilhali ni njia ya kuwakandamiza zaidi,” alisema.
“Unazungumza nini na mtu ambaye amekukalia koo? Ninamwambia Raila sasa hadharani: tafadhali jitoe. Acha damu kumwagika. Wakenya watajitatua wenyewe.”