NAIROBI, KENYA, Jumanne, Novemba 18, 2025 – Jumuiya ya Rastafari ya Kenya imefufua upya shinikizo la kutambuliwa kwa matumizi ya bangi kama sehemu ya ibada yao, wakati Mahakama Kuu ikiweka tarehe za usikilizwaji wa kesi yao ya kikatiba inayodai kukiukwa kwa haki za kuabudu, faragha na usawa.
Jumuiya hiyo inasema kwa miaka mingi imebaguliwa kwa sababu ya kutumia bangi katika ibada na mila zao za kiroho.
Mmoja wa wazee alisema mbele ya waandishi: “Mungu ndiye aliweka bangi duniani kwa matumizi ya kiroho. Haitakiwi kutupeleka selo kwa sababu ya imani.”
Akaongeza: “Kuna dawa hatari huko nje, lakini ni sisi wanaonyoshewa kidole. Tunajiuliza: kwa nini bangi ya ibada inachukuliwa kama kosa?”
Kwa Rastafari, bangi ni kifungo cha kijamii na cha kiimani, si kinyume cha sheria.
Mahakama Kuu Yapanga Tarehe Mpya za Kesi
Kesi hiyo itasikizwa Januari 14 na 15, 2026.
Jumuiya ya Rastafari ya Kenya inasema hatua hiyo inawapa nafasi kueleza namna vifungu vya sasa vinavyoruhusu kukamatwa kwa watumiaji wa bangi vinavyokiuka Katiba.
Katika hati za mahakama, wanadai: “Hakuna mtu anayepaswa kukamatwa kwa kutumia bangi nyumbani kwake au kwenye ibada, kwa sababu hiyo ndiyo imani yake.”
Wanasema vifungu hivyo vinavunja haki ya faragha chini ya Kifungu cha 31(a) na uhuru wa kuabudu chini ya Kifungu cha 32,
Wanasheria Wasema Rastafari Wana Baguliwa
Mawakili wa Jumuiya, Shadrack Wambui na Danstan Omari, waliambia wanahabari kuwa suala hili halihusu anasa bali uhuru wa kidini.
Omari alisema: “Kama Wahindu au Njuri Ncheke wanafanya ibada zao kwa amani, kwa nini Rastafari wafanyiwe ukatili kwa kutumia bangi ya kiibada?”
Wambui naye aliongeza: “Hatuombi bangi itumike kiholela. Tunaomba tu watumishi wa imani hii walindwe sawa na waumini wengine.”
Mandhari ya Utamaduni Nje ya Mahakama
Waumini wa Rastafari walijitokeza kwa makundi nje ya mahakama wakiimba na kushangilia utambulisho wao.
Wakiwa wamevalia rangi za kijani, dhahabu na nyekundu, walibeba vibuyu na alama za kitamaduni zilizoashiria amani na mshikamano.
Walipaza sauti: “Sayansi ilianzia Afrika! Turudi kwenye mizizi ya kale!” Huku wakiimba nyimbo za Rastafari zilizoelezea umoja wa Kiafrika.
Walibeba pia bendera ya Kenya, ya Umoja wa Afrika na ile ya Black supremacy, wakisema mapambano yao ni ya hadhi na heshima.
Ombi la Kuundwa kwa Jopo Maalum la Majaji
Jumuiya ya Rastafari ya Kenya inataka Jaji Mkuu ateue jopo la majaji kutokana na uzito wa hoja zao.
Wanadai kesi yao inagusa swali la msingi: Je, imani inayotumia bangi inaweza kuchukuliwa kama kosa la jinai?
Katika maombi yao, wanasema: “Kesi hii haihusu kuvuta bangi ovyo. Inahusu haki ya kuishi kulingana na imani yako bila kuonewa.”
Safari ya Miaka Mingi
Jumuiya hiyo iliwasilisha ombi la kwanza mwaka 2021, wakitaka kusitishwa kwa vifungu vinavyoruhusu kukamatwa kwa waumini wanaotumia bangi nyumbani au mahali pa ibada.
Wanadai kukamatwa na kushtakiwa kumewafanya waumini wajione wakosaji katika nchi yao wenyewe, kinyume na matakwa ya Katiba.
Kwa Rastafari, bangi si burudani wala uhalifu. Ni sehemu ya ibada na utambulisho wao. Na mwaka 2026 huenda ukawa mwanzo wa majibu ambayo wameyangoja kwa muda mrefu.



© Radio Jambo 2024. All rights reserved