logo

NOW ON AIR

Listen in Live

CS Ogamba: Butere Girls walipewa fursa ya kupanda jukwaani 8a.m, walikataa wenyewe!

"Hivyo wanafunzi kwa hiari yao tu walisema hawawezi kuonyesha mchezo wao,” Ogamba alisisitiza.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Hivi Punde10 April 2025 - 13:07

Muhtasari


  • CS Ogamba alieleza kwamba mmoja wa wanafunzi hao alijongea mbele baada ya kuimba wimbo wa taifa na kusema kwamba hawangeweza kuonyesha igizo lao bila ya kuwepo kwa mkurugenzi wao, Cleophas Malala.
  • “Na Bwana Malala si Mwalimu katika shule ya Butere, yeye si mkurugenzi katika shule ya Butere na hata si muongozaji wa igizo hilo."
  • "Hivyo wanafunzi kwa hiari yao tu walisema hawawezi kuonyesha mchezo wao,” Ogamba alisisitiza.

Julius Ogamba Migos, Waziri wa Elimu//X

WAZIRI wa Elimu, Julius Ogamba Migos amewanyooshea wanafunzi wa shule ya upili ya wasichana ya Butere kidole cha lawama kwa kukataa kuonyesha maigizo yao licha ya kupewa fursa ya kupanda jukwaani.

Akizungumza katika kaunti ya Nakuru adhuhuri ya Alhamisi kufuatia tukio hilo ambalo limeacha taifa katika gumzo kubwa, Ogamba alisema kwamba wanafunzi hao walikataa wenyewe kuonyesha igizo lao la ‘Echoes of War’ licha ya kukubaliwa na hata kuitwa kupanda jukwaani.

Kwa mujibu wa Waziri Ogamba, wanafunzi hao walipewa fursa ya kupanda jukwaani majira ya saa mbili asubuhi ya Alhamisi ili kutoa onyesho lao, lakini baada ya kufika jukwaani, waliimba wimbo wa taifa na kuondoka.

CS Ogamba alieleza kwamba mmoja wa wanafunzi hao alijongea mbele baada ya kuimba wimbo wa taifa na kusema kwamba hawangeweza kuonyesha igizo lao bila ya kuwepo kwa mkurugenzi wao, Cleophas Malala.

Ogamba hata hivyo alihoji Malala alikuwa na umuhimu gani wa kuwepo katika ukumbi ili igizo hilo kuendelea, akisema kwamba yeye si Mwalimu wala mkurugenzi katika shule ya Butere Girls.

“Tuna ufahamu wa kutosha kwamba wanafunzi walipewa fursa ya kuonyesha mchezo wao majira ya saa mbili asubuhi. Wakati walifika ukumbini na baada ya kuimba wimbo wa taifa, mmoja wao alijongea mbele na kusema kwamba hawako tayari kucheza igizo lao bila ya mkurugenzi wao, bwana Malala.”

“Na Bwana Malala si Mwalimu katika shule ya Butere, yeye si mkurugenzi katika shule ya Butere na hata si muongozaji wa igizo hilo. Hivyo wanafunzi kwa hiari yao tu walisema hawawezi kuonyesha mchezo wao,” Ogamba alisisitiza.

Kuhusu suala la vurugu kutoka kwa polisi ambao wanasemekana kutupa vitoza machozi katika shule walimofanya makaazi yao ya muda wasichana wa Butere, Ogamba alisema kwamba hana Habari kuhusu hilo huku akiahidi kutoa taarifa baada ya kuarifiwa na mamlaka husika.

Mchezo wa kuigiza wa ‘Echoes of War’ ambao uliandikwa na aliyekuwa seneta wa Kakamega Cleophas Malala umekuwa gumzo katika siku za hivi karibuni haswa baada ya kupigwa marufuku na kusababisha suala hilo kuishia mahakamani.

Mahakama ilitoa uamuzi wa mchezo huo wa kuigizwa kuendelea bila kuhitilafiwa na yeyote, lakini siku moja kabla ya siku ya maonyesho katika kaunti ya Nakuru, vurumai zilizuka, Malala akiripotiwa kuzuia kuingia katika eneo walimokuwa wanafunzi hao.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved