Delcat Idengo aliuawa akiwa katika utayarishaji wa video ya muziki mjini Goma, eneo la mashariki mwa DRC.
Mauaji ya Idengo yanahusishwa na mzozo huu, hasa kwa kuwa wimbo wake mpya "Bunduki".
Delcat Idengo aliuawa Goma
Mwanamuziki mashuhuri kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Delphin Katembo Vinywasiki, anayefahamika kwa jina la kisanii Delcat Idengo, ameuawa akiwa katika utayarishaji wa video ya muziki mjini Goma, eneo la mashariki mwa DRC linalokumbwa na mzozo wa kivita.
Mwili wake ulipatikana siku ya Alhamisi ukiwa na majeraha kichwani, huku ripoti ambazo bado hazijathibitishwa zikidai kwamba aliuawa kwa kupigwa risasi.
Idengo alikuwa mwanamuziki anayejulikana kwa nyimbo zake za kukosoa serikali na waasi, na hivi majuzi alikuwa ametoroka gereza la Goma, baada ya wanamgambo wa M23 kuuteka mji huo mnamo Januari.
Eneo la Mashariki mwa DRC linakabiliwa na mapigano kati ya jeshi la serikali na makundi yenye silaha, yanayoshindania udhibiti wa eneo hilo lenye utajiri mkubwa wa madini kama dhahabu, cobalt na coltan.
Katika mzozo huu, kundi la M23, linalodaiwa kuungwa mkono na Rwanda, limeendelea kuiteka miji muhimu, ikiwemo Goma.
Mauaji ya Idengo yanahusishwa na mzozo huu, hasa kwa kuwa wimbo wake mpya "Bunduki" ulikuwa unalaani uvamizi wa waasi.
Serikali ya Congo, kupitia msemaji wake Patrick Muyaya, ililaani mauaji hayo, ikisema ni "kitendo cha kuchukiza," huku ikiilaumu M23 kwa kuhusika.
Hata hivyo, M23 imekanusha shutuma hizo, badala yake ikidai kuwa wapiganaji wanaounga mkono serikali ndio waliohusika na mauaji hayo.
Kwa mujibu wa ripoti za Umoja wa Mataifa (UN), mapigano ya hivi karibuni yamesababisha vifo vya takriban watu 2,900, huku zaidi ya 700,000 wakilazimika kuyakimbia makazi yao.
Tukio hili linaongeza taharuki zaidi katika eneo la Goma, huku vita vikiendelea kati ya serikali ya Félix Tshisekedi na waasi wa M23, katika mgogoro unaotishia uthabiti wa kanda ya Maziwa Makuu.