Baadhi ya MCA wa Kiambu wamtetea Gavana Wamatangi, watupilia mbali shinikizo la kumtimua

Haya yanajiri siku moja tu baada ya wawakilishi Wadi wa Kaunti ya Kiambu kumpa Gavana siku 21 kujibu tuhuma zilizoelekezwa kwake au atimuliwe.

Muhtasari

•Mwakilishi wa Wadi ya Kameno Peter Mburu, alipuuzilia mbali ripoti hizo akidai kuwa tuhuma zilizopendekezwa dhidi ya Wamatangi zilikuwa zikiongozwa na baadhi ya watu wa kutoka nje.

 

GAVANA KIMANI WAMATANGI

Kundi moja la wakilishi wadi wa kaunti ya Kiambu limepuuzilia mbali ripoti zinazodai kuwa wanataka kumtimua Gavana Kimani Wamatangi.

Haya yanajiri siku moja tu baada ya wakilishi Wadi wa Kaunti ya  Kiambu kumpa Gavana siku 21 kujibu tuhuma dhidi  yake au atimuliwe.

Wakilishi wadi hao  walilalamika kwamba juhudi zao za kutaka Gavana aunde baraza la mawaziri linalojumuisha wote zilipuuzwa, pia walitaka Wamatangi kuteua mameneja wa manispaa sita za Kiambu ambazo wanasema ziko katika hatari kupoteza ufadhili wa Shilingi  bilioni 1.3 kila mwaka, kutoka Benki ya Dunia.

Zaidi ya hayo, MCAs waliitaka Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) na DCI kuanzisha uchunguzi wa jinsi mabilioni ya pesa za umma yametumika chini ya uongozi wa Wamatangi.

Kwenye kikao na wanahabari siku ya Alhamisi, Mwakilishi wa Wadi ya Kameno Peter Mburu, alipuuzilia mbali ripoti hizo akidai kuwa tuhuma dhidi ya Wamatangi zimechochewa na baadhi ya watu kutoka nje.

"Tatizo kubwa tunalokumbana nalo katika kaunti ya Kiambu ni ushawishi wa  kutoka pande tofauti. Tuna wanasiasa wengine, tuna wanakandarasi, madalali na watu wengine ambao wanavuruga bunge la kaunti ya Kiambu," Mburu alisema.

"Makataa haya yangeshughulikiwa vyema ndani ya mfumo wa kisheria wa bunge. Kwa hivyo ikiwa mwanachama yeyote ana maswali kuhusu suala la serikali ya kaunti, njia bora ni kufanya hivyo kupitia muundo wa bunge sio kupitia mitandao ya kijamii,"aliongeza.