
Aliyekuwa Naibu Rais wa Kenya, Rigathi Gachagua, amezua hisia mseto baada ya kumuidhinisha waziri mkuu wa zamani Raila Odinga kwa nafasi ya Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika (AUC).
Katika taarifa yake siku ya Ijumaa asubuhi, Gachagua alisema kuwa Raila Odinga ndiye mgombea anayefaa zaidi kushikilia nafasi
Alisisitiza kuwa bara la Afrika linahitaji uongozi wake thabiti.
"Mheshimiwa Raila Odinga ndiye chaguo bora kwa uenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika. Afrika inastahili uongozi bora, na hakuna shaka kuwa Raila ana maono mapana na amekuwa mtetezi wa maslahi ya Waafrika kwa muda mrefu," alisema Gachagua kupitia Facebook.
DP huyo wa zamani aliongeza kuwa Raila ni kiongozi anayeweza kuunganisha mataifa ya Afrika yanayozungumza Kiingereza (Anglophone) na Kifaransa (Francophone) ili kujenga mshikamano wa bara lenye umoja na mwelekeo wa pamoja kwa mustakabali wake.
"Kama bara, tunahitaji mtu wa kaliba ya Raila Odinga kuunganisha Afrika kuelekea mustakabali wa pamoja," alisisitiza.
Gachagua alibainisha kuwa ushindi wa Raila katika uchaguzi wa AUC jijini Addis Ababa utakuwa ishara ya kuendeleza ari yake ya Uafrika, ambayo ameishi nayo na kuitetea kwa miaka mingi.
"Ushindi wa Raila Odinga utakuwa hatua muhimu kwa maendeleo ya Afrika. Hili litakuwa pia ni fahari kwa Kenya, taifa letu la kuzaliwa," alisema.
Wakati baadhi ya Wakenya wanaona hatua hii kama ishara ya umoja na kuweka maslahi ya bara mbele, wengine, wanabaki na shaka, wakikumbuka historia ya ushindani wa kisiasa kati ya viongozi hawa wawili.
Kwenye mitandao ya kijamii, maoni yamegawanyika. Baadhi ya
watumiaji wanasifu hatua ya Gachagua, wakiona kama ishara ya kuweka maslahi ya
Afrika mbele ya tofauti za kisiasa.
Kwa mfano, mtumiaji mmoja aliandika, "Kumuunga mkono Raila ni ishara ya kuweka umoja wa Afrika mbele; siasa kando."
Kwa upande mwingine, wapo wanaohoji uhalisia wa uungwaji mkono huu, wakikumbuka ushindani mkali wa kisiasa uliokuwepo kati ya Gachagua na Odinga.
Mchanganuzi mmoja wa kisiasa alibainisha, "Je, huu ni uungwaji mkono wa kweli au ni mbinu za kisiasa? Ikizingatiwa historia yao, ni vigumu kusema."
Wachambuzi wa kisiasa wanasema kuwa hatua hii inaweza kuwa na maana kubwa katika siasa za Kenya na bara la Afrika kwa ujumla. Inaweza kuashiria mabadiliko ya kimkakati yanayolenga kuimarisha ushawishi wa Kenya ndani ya Umoja wa Afrika na kukuza umoja wa kitaifa.
Uchaguzi wa Mwenyekiti wa AUC unatarajiwa kufanyika Jumamosi, Februari 15, jijini Addis Ababa, Ethiopia.
Odinga atachuana na Mahamoud Ali Youssouf wa Djibouti na Richard Randriamandrato wa Madagascar katika kinyang'anyiro hiki.
Matokeo ya uchaguzi huu yanatarajiwa kwa hamu kubwa, huku uungwaji mkono wa Gachagua ukiongeza mvuto mpya katika mchakato huu.