logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Rais Ruto aongoza viongozi wakuu kumuaga Wafula Chebukati Kiminini, Trans Nzoia

Mamia ya waombolezaji wamekusanyika kutoa heshima zao za mwisho kwa kiongozi huyo zamani wa IEBC.

image
na Samuel Mainajournalist

Yanayojiri08 March 2025 - 11:50

Muhtasari


  •  Miongoni mwa viongozi mashuhuri waliohudhuria ni Rais Ruto,  Mudavadi, Wetang’ula, Kingi,  Gavana Lusaka, na Gavana George Natembeya.
  • Chebukati atazikwa katika shamba lake la Sabata, Kitale, Kaunti ya Trans Nzoia.

Rais William Ruto akaribishwa Kiminini na Gavana George Natembeya mnamo Machi 8, 2025.

Mazishi ya aliyekuwa mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), Wafula Chebukati, yanaendelea hivi sasa katika eneo la Kiminini, Kaunti ya Trans Nzoia, huku viongozi wa kitaifa, jamaa, marafiki, na mamia ya waombolezaji wakikusanyika kutoa heshima zao za mwisho kwa kiongozi huyo aliyekuwa na mchango mkubwa katika kusimamia chaguzi nchini

 Miongoni mwa viongozi mashuhuri waliohudhuria ni Rais William Ruto, Waziri Mkuu Musalia Mudavadi, Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula, Spika wa Seneti Amason Kingi, Gavana wa Bungoma Ken Lusaka, Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya, Katibu wa Usalama wa Ndani Raymond Omollo, pamoja na wabunge kadhaa. Pia, aliyekuwa Waziri wa Afya Susan Nakhumicha ni miongoni mwa waliokuja kuomboleza. 

Chebukati atazikwa katika shamba lake la Sabata, Kitale, Kaunti ya Trans Nzoia. Mwili wake uliwasili katika uwanja wa ndege wa Kitale Alhamisi jioni, Machi 6, 2025, ambapo ulipokelewa na familia, marafiki na viongozi wa kisiasa.  

Mazishi haya yanajiri siku chache baada ya ibada ya kumbukumbu iliyofanyika katika kanisa la CITAM Karen, ambapo familia, marafiki, na viongozi walimsifu Chebukati kwa maisha yake ya maadili na uadilifu katika utumishi wa umma.

Chebukati alihudumu kama mwenyekiti wa IEBC kwa kipindi cha miaka sita, akisimamia uchaguzi mkuu wa 2017, marudio ya uchaguzi wa urais wa mwaka huo, na uchaguzi mkuu wa 2022.

Alijulikana kwa msimamo wake wa kuzingatia sheria, na licha ya changamoto nyingi alizokumbana nazo, alihakikisha kuwa matokeo ya uchaguzi yanatangazwa kwa mujibu wa katiba. 

Katika uchaguzi wa 2022, alikabiliwa na shinikizo kubwa wakati wa kutangaza mshindi wa urais, lakini alisimama imara akisisitiza kuwa tume hiyo ilifuata taratibu zote za kisheria. Hatua yake ilizua mijadala mikali ya kisiasa, lakini wengi walimtambua kama mtetezi wa ukweli na haki. 

Mbali na kazi yake katika IEBC, Chebukati alikuwa mume na baba wa watoto watatu—Jonathan, Emmanuel, na Rachel. Wakati wa ibada ya kumbukumbu jijini Nairobi, familia yake ilimtaja kama baba mwenye nidhamu, upendo, na mshauri mzuri kwao.

 Emmanuel, mwanawe wa pili, alielezea jinsi baba yao alivyowahimiza kuwa na bidii na kutanguliza maadili maishani mwao. 

"Baba alikuwa mtu wa mpangilio na mwenye msimamo. Alitufundisha kuwa maadili na ukweli ni nguzo muhimu katika maisha," alisema Emmanuel. 

Mazishi ya Chebukati yanaendelea, huku viongozi na waombolezaji wakiendelea kutoa heshima zao za mwisho.

 

Kifo chake mnamo Februari 20 kutokana na mshtuko wa moyo kimeacha pengo kubwa katika sekta ya uchaguzi na utawala wa kidemokrasia nchini.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved