logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mwanahabari wa KBC apatikana akiwa amefariki

KBC imemtaja marehemu Fredrick kama mtu aliyejituma kwa kazi yake.

image
na Japheth Nyongesa

Yanayojiri21 March 2025 - 14:07

Muhtasari


  • Wasimamizi wa kitua hicho wametangaza kuwa marehemu alifariki Ijumaa, Machi 21.
  • Amepatikana akiwa amefariki nyumbani kwake katika eneo bunge la Kinoo, kaunti ya Kiambu.

Mwanahabari Fredrick Parsayo 

Shirika la utangazaji nchini KBC  limeamkia maombolezo kufuatia kifo cha Fredrick Parsayo, mwandishi wa habari ambaye amekuwa akihudumu katika kitengo cha uhariri.

Wasimamizi wa kitua hicho wametangaza kuwa marehemu alifariki Ijumaa, Machi 21, nyumbani kwake katika eneo la Kinoo, kaunti ya Kiambu.

Kulingana na shirika la habari, mwandishi huyo wa habari alikufa kwa njia  isiyoeleweka na tayari maafisa wa usalama wameanzisha uchunguzi wa kina kubaini chanzo cha kifo.

"Ni kwa moyo mzito kwamba tunatangaza habari za kifo cha mwenzetu mpendwa, Fredrick Parsayo  ambaye amekuwa  mwandishi wa habari katika Idara ya Wahariri ya KBC," sehemu ya taarifa ya KBC ilisoma.

Fredrick ametuacha kwa huzuni Ijumaa, Machi 21, 2025, chini ya hali ambazo bado zinachunguzwa, nyumbani kwake katika eneo bunge la Kinoo-Kikuyu. Jambo hili lisilotarajiwa limetuathiri sana sisi sote," taarifa hiyo iliongeza.

Tukio hilo limeripotiwa katika Kituo cha Polisi cha Kinoo, na mwili wa marehemu ulipelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha St Teresa huku familia yake ikiwa tayari imearifiwa kuhusu kifo chake.

KBC imemtaja Fredrick mtu aliyejituma kwa kazi yake na kusaidia pakubwa kwenye kitengo cha uhariri kwenye shirika hilo la habari.

"Kwa niaba ya Bodi ya Wakurugenzi ya KBC, Usimamizi, na wafanyikazi wetu wote, tunatoa rambirambi zetu za dhati kwa familia ya Fredrick, marafiki, na wale wote walioathiriwa na kifo chake," shirika la habari lilitangaza.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved