logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Timu ya Barcelona yapatwa na msiba, mchuano wa Laliga wapanguliwa

Kifo hicho kilitokea muda mfupi kabla ya mechi ya Laliga dhidi ya Osasuna, iliyokuwa imepangwa kuchezwa Jumamosi.

image
na Samuel Mainajournalist

Football09 March 2025 - 08:33

Muhtasari


  • Kutokana na msiba huu, uongozi wa FC Barcelona, kwa kushirikiana na Osasuna na maafisa wa La Liga, waliamua kuahirisha mechi.
  •  Kifo cha Miñarro García kimezua maombolezo makubwa ndani ya klabu.

Barcelona imepatwa na msiba

Klabu ya FC Barcelona imepatwa na msiba mzito baada ya kifo cha ghafla cha daktari wao wa timu ya kwanza, Carles Miñarro García, mwenye umri wa miaka 50.

Tukio hilo la kuhuzunisha lilitokea muda mfupi kabla ya mechi yao ya La Liga dhidi ya Osasuna, iliyokuwa imepangwa kuchezwa Jumamosi katika Uwanja wa Estadi Olímpic Lluís Companys.

Miñarro García alijiunga na timu ya matibabu ya FC Barcelona msimu uliopita na alikuwa akiheshimiwa sana na wachezaji pamoja na wafanyakazi wenzake.

Kifo chake kimeacha pengo kubwa ndani ya klabu, na kusababisha maombolezo makubwa miongoni mwa wachezaji, viongozi, na mashabiki.

Kutokana na msiba huu, uongozi wa FC Barcelona, kwa kushirikiana na Osasuna na maafisa wa La Liga, waliamua kuahirisha mechi hiyo.

Katika taarifa yao rasmi, klabu hiyo ilieleza huzuni yao kubwa kwa kuondokewa na mtaalamu huyo wa tiba ya michezo.

"FC Barcelona inasikitika kutangaza kifo cha daktari wa timu ya kwanza, Carles Miñarro García, jioni ya leo. Kutokana na hili, mchezo kati ya FC Barcelona na CA Osasuna umeahirishwa hadi tarehe nyingine.

Bodi ya Wakurugenzi ya FC Barcelona na wafanyakazi wote tunatoa rambirambi zetu za dhati kwa familia na marafiki zake katika kipindi hiki kigumu," taarifa ilisomeka.

 Taarifa hii iliwasilishwa kwa mashabiki waliokuwepo uwanjani, takriban dakika 15 kabla ya mchezo kuanza, na kusababisha mshtuko mkubwa kwa wote waliokuwepo.

 Kifo cha Miñarro García kimezua maombolezo makubwa ndani ya klabu. Rais wa FC Barcelona, Joan Laporta, alisema:

 "Kifo cha ghafla cha Carles ni pigo kubwa kwetu sote. Alikuwa mtu muhimu sana katika timu yetu, na mchango wake hautasahaulika."

 Wachezaji wa Barcelona pia walionyesha huzuni yao kupitia mitandao ya kijamii, wakielezea namna daktari huyo alivyokuwa sehemu muhimu ya timu na jinsi walivyompenda.

Baada ya mashauriano kati ya pande husika, mechi ya Barcelona dhidi ya Osasuna iliakhirishwa rasmi. Hadi sasa, La Liga bado haijatangaza tarehe mpya ya mchezo huo.

 

Kwa sasa, FC Barcelona inajikita katika maandalizi ya mechi yao ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya Benfica, inayotarajiwa kufanyika Jumanne ijayo.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved